TANZANIA YAZINDUA UWANJA WA KISASA WA KRIKETI, ICC YAIONA TAYARI KWA MASHINDANO YA KIMATAIFA


Mwenyekiti wa Shirikisho la Kimataifa la Kriketi (ICC), Jay Shah (katikati), akiongoza uzinduzi wa Uwanja wa Kisasa wa Chama cha Kriketi Tanzania (TCA Cricket Arena) uliojengwa katika Viwanja vya Michezo vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Uwanja huo utatumika kama kituo cha taifa cha kukuza vipaji na kuandaa timu za taifa za wanaume, wanawake na vijana wenye umri wa chini ya miaka 19. Wengine pichani ni wadau wa mchezo wa kriketi.

DAR ES SALAAM – Shirikisho la Kimataifa la Kriketi (International Cricket Council - ICC) limesema Tanzania ina nafasi ya kuwa miongoni mwa mataifa yatakayoweza kuandaa mashindano makubwa ya kriketi duniani siku zijazo, kufuatia uwekezaji unaoendelea katika miundombinu ya kisasa ya mchezo huo na maendeleo ya vijana.

Kauli hiyo imetolewa wakati wa uzinduzi wa Uwanja wa Kisasa wa Chama cha Kriketi Tanzania (TCA Cricket Arena), uliojengwa katika viwanja vya michezo vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Uwanja huo utatumika kama kituo cha taifa cha kukuza vipaji na kuandaa timu za taifa za wanaume, wanawake na vijana wenye umri wa chini ya miaka 19.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi, Mwenyekiti wa ICC, Jay Shah, alisema Tanzania imeonyesha dhamira kubwa ya kuendeleza mchezo wa kriketi kupitia uwekezaji katika miundombinu na programu za maendeleo ya vijana, hatua ambayo imeifanya kuwa miongoni mwa mataifa yanayokua kwa kasi katika mchezo huo barani Afrika.

Alisema iwapo kasi hiyo ya maendeleo itaendelea, Tanzania inaweza kuwa miongoni mwa nchi zitakazopewa fursa ya kuandaa mashindano makubwa ya kimataifa, ikiwemo Kombe la Dunia la Kriketi, katika miaka ijayo.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Chama cha Kriketi Tanzania (Tanzania Cricket Association - TCA), Hamisi Hassan Abdallah, alisema uwanja huo mpya utaongeza uwezo wa Tanzania kuandaa mashindano ya kimataifa huku ukiwapatia wachezaji mazingira bora ya mazoezi yanayokidhi viwango vya kimataifa.

Alibainisha kuwa kwa muda mrefu TCA ilikuwa na uwanja mmoja pekee, hali iliyokuwa ikizuia juhudi za kuandaa mashindano makubwa kutokana na uhaba wa miundombinu inayokidhi matakwa ya mashirikisho ya kimataifa.

Naye Afisa Mwandamizi wa Michezo kutoka Baraza la Michezo la Taifa (NSC), Apansia Lema, alisema Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya michezo ili kuibua na kukuza vipaji vya vijana nchini.

Alisema maendeleo ya mchezo wa kriketi yanaendelea kuimarika, huku zaidi ya shule 400 nchini zikishiriki mchezo huo. Aidha, alitaja kufuzu kwa timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 19 kushiriki Kombe la Dunia la Kriketi 2026 kuwa mafanikio makubwa yanayoonyesha mwelekeo mzuri wa maendeleo ya mchezo huo nchini.

Uzinduzi wa TCA Cricket Arena unatarajiwa kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha kriketi katika ukanda wa Afrika Mashariki na kuongeza uwezo wa nchi kuvutia mashindano ya kimataifa, kuendeleza vipaji vya vijana na kukuza utalii wa michezo.


Share:

BENKI ZA ABSA NA TCB KUIMARISHA MAHUSIANO YA USHIRIKIANO WA KIMKAKATI

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akisalimiana na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake, jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto), akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo (kushoto), pamoja na baadhi ya maofisa wa benki hiyo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa nne kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo (wa tano kushoto), pamoja na baadhi ya maofisa kutoka benki zote mbili, wakipiga picha ya kumbukumbu mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kutembelea ofisini za TCB, jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.
Share:

BENKI ABSA TANZANIA YAENDELEA KUJIZATITI KUTOA HUDUMA BORA KWA WATEJA

Mtendaji Mkuu wa Kitengo Cha Wateja wa Makampuni (CIB), wa Absa Group kutoka Afrika Kusini, Bw. Zaid Moola (wa pili kulia), akizungumza na baadhi ya wateja wa makampuni (CIB), katika hafla iliyoandaliwa na Benki ya Absa Tanzania jijini Dar es Salaam leo, kama sehemu ya kudumisha ushikiriano wa kibiashara baina yao. kikao hicho pia kiliwakutanisha wateja hao na watendaji wakuu wa kitengo cha CIB kutoka Absa Group, waliopo nchini kwa ziara ya kikazi.

Katika kuendeleza ushirikiano na kutambua mchango mkubwa wa wateja wake wa Kitengo cha Corporate and Investment Banking (CIB), Benki ya Absa Tanzania leo imeandaa kikao cha kifungua kinywa cha kukutanisha wadau wa biashara jijini Dar es Salaam.

Kikao hicho kimetoa fursa kwa viongozi wa benki na wateja kufanya majadiliano ya wazi kuhusu fursa za ukuaji wa biashara, mwenendo wa masoko, pamoja na mustakabali wa sekta ya biashara nchini Tanzania.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser, amesema benki hiyo inaendelea kutoa huduma mbalimbali za kifedha zinazolenga kukidhi mahitaji ya wateja wake, hususan makampuni na taasisi zinazofanya biashara kubwa.

Aidha, hafla hiyo ilitumika kuwatambulisha viongozi waandamizi kutoka Kitengo cha Corporate and Investment Banking cha Absa Group, wakiongozwa na Mtendaji Mkuu wake, Bw. Zaid Moola, ambao walipata nafasi ya kukutana na kufanya mazungumzo ya moja kwa moja na wateja wakati wa ziara yao ya kikazi nchini Tanzania.

Ziara ya viongozi hao wa Absa Group inaonesha dhamira ya benki hiyo ya kuendelea kuimarisha mahusiano na wateja wake pamoja na kutoa suluhisho bunifu za kifedha zitakazosaidia biashara kukua na kustawi.

Hatua hiyo pia inaakisi dira ya Absa ya "Kuwezesha Afrika ya Kesho, Pamoja... Hadithi Moja Baada ya Nyingine."
Mtendaji Mkuu wa Kitengo cha Wateja wa Makampuni (CIB), wa Absa Group Kutoka Afrika Kusini, Bw. Zaid Moola (katikati), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kulia) na Mkurugenzi Mtendaji wa Wateja wa Makampuni wa Kanda ya Afrika, Bw. Sola Adegbesan, wakifurahi katika hafla iliyoandaliwa na Benki ya Absa jijini Dar es Salaam leo kwa wateja wa makampuni, kama sehemu ya kudumisha ushikiriano wa kibiashara baina yao. kikao hicho pia kiliwakutanisha wateja hao na watendaji hao kutoka absa group, waliopo nchini kwa ziara ya kikazi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kulia), akimsikiliza Ofisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi inayotoa huduma za kifedha ya ASA Microfinance, Bw. Muhammad Shah Newaj, katika hafla iliyoandaliwa na benki hiyo kwa wateja wake wa makampuni (CIB), jijini Dar es Salaam leo, kama sehemu ya kudumisha ushirikiano wa kibiashara baina yao. Kikao hicho pia kiliwakutanisha wateja hao na watendaji wakuu wa CIB kutoka Absa Group, waliopo nchini kwa ziara ya kikazi. Katikati ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Masoko ya Fedha za Kigeni wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Irene Rwegalulira.
Mkurugenzi wa Masoko na Mahusiano wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Aron Luhanga akizungumza katika hafla waliyowaandaliwa wateja wa makampuni (CIB), jijini Dar es Salaam leo, kama sehemu ya kudumisha ushikiriano wa kibiashara baina yao. kikao hicho pia kiliwakutanisha wateja hao na watendaji wakuu wa kitengo cha CIB kutoka Absa Group, waliopo nchini kwa ziara ya kikazi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto), akimsikiliza Mkurugenzi wa Kitengo cha Masoko ya Fedha za Kigeni wa benki hiyo, Bi. Irene Rwegalulira, wakati wa hafla iliyoandaliwa na benki hiyo kwa wateja wake wa makampuni (CIB), jijini Dar es Salaam leo. Wengine kutoka Kushoto ni Mkurugenzi wa Wateja wa Makampuni wa Absa Tanzania, Bi. Nellyana Mmanyi, Mkurugenzi wa Masoko na Mahusiano, Bw. Aron Luhanga na Mkuu wa Kitengo cha Shughuli za kibenki wa benki hiy, Bw. Alred Urasa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Wateja wa Absa Group, Bw. Clive Potter (kushoto), akizungumza na baadhi ya wateja wa makampuni (CIB), katika hafla iliyoandaliwa na Benki ya Absa Tanzania jijini Dar es Salaam leo, kama sehemu ya kudumisha ushikiriano wa kibiashara baina yao. Katikati ni Mkurugenzi wa Fedha wa Amref Health Africa, Bw. Damas Nugashe na Mkurugenzi Mtendaji wa Savanna Fibre Tanzania, Bw. Thomas Wenanga.
Mtendaji Mkuu wa Wateja wa Makampuni (CIB) wa Absa Group, Bw. Zaid Moola, baadhi ya watendaji wakuu kutoka Absa Group, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser, baadhi ya wafanyakazi na wateja wa CIB, wakipiga picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa kikao hicho jijini Dar es Salaam leo.
Share:

WAZIRI MASAUNI AONGOZA SAVE SOIL WALKATHON, ATOA WITO WA KULINDA UDONGO NA MAZINGIRA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, ameongoza mamia ya wananchi na wadau mbalimbali wa mazingira katika matembezi ya Save Soil Walkathon, huku akitoa wito kwa Watanzania kushiriki kikamilifu katika juhudi za kulinda udongo na mazingira kwa ajili ya maendeleo endelevu ya taifa.

Mhe. Masauni, ambaye alikuwa mgeni rasmi wa tukio hilo, alishiriki matembezi hayo yaliyoandaliwa na Lions Club of Dar es Salaam Mazingira chini ya kaulimbiu ya “Save Soil, Save Our Future” (Linda Udongo, Linda Mustakabali Wetu).
Tukio hilo liliwakutanisha wadau wa mazingira, taasisi mbalimbali, sekta binafsi na wananchi katika kampeni ya kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kuhifadhi afya ya udongo na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.

Akizungumza baada ya matembezi hayo, Mhe. Masauni alisema afya ya udongo ni msingi wa usalama wa chakula, uhifadhi wa mazingira na ustawi wa uchumi wa taifa, hivyo kuna umuhimu wa kila Mtanzania kushiriki katika juhudi za kuutunza.

"Udongo ni rasilimali muhimu inayobeba maisha yetu ya kila siku. Bila udongo wenye afya hatuwezi kuwa na usalama wa chakula, mazingira bora wala maendeleo endelevu. Ni wajibu wa kila Mtanzania kushiriki katika juhudi za kulinda mazingira na kutumia ardhi kwa njia zinazohifadhi uhai wake kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho," alisema Mhe. Masauni.

Katika kuonesha kwa vitendo dhamira ya kulinda mazingira, Mhe. Masauni pia alipanda mti ikiwa ni ishara ya kujitolea katika uhifadhi wa udongo na mazingira pamoja na kuhamasisha wananchi kushiriki katika upandaji miti kama sehemu ya juhudi za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa ardhi.
Kwa upande wake, Rais wa Lions Club of Dar es Salaam Mazingira, Lion Ramadevi, alisema Save Soil Walkathon ni sehemu ya kampeni pana inayolenga kuhamasisha jamii kutambua mchango mkubwa wa udongo katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kimazi-ngira.

"Save Soil Walkathon si matembezi pekee, bali ni harakati ya kuhamasisha mabadiliko ya tabia na kuwajengea wananchi uelewa wa umuhimu wa kulinda udongo. Tunataka kuona jamii, taasisi na sekta binafsi zikichukua hatua za pamoja katika kuhifadhi mazingira kwa mustakabali wa taifa letu," alisema Lion Ramadevi.

Naye Esther Msuya, Meneja wa Afya, Usalama, Ulinzi na Mazingira (HSSE) wa GSG Energies, alisema kampuni hiyo itaendelea kuunga mkono mipango na kampeni zinazolenga uhifadhi wa mazingira na maendeleo endelevu nchini.

"Kulinda mazingira ni jukumu la kila mmoja wetu. GSG Energies tunaamini kuwa maendeleo ya kweli lazima yaende sambamba na uhifadhi wa mazingira."

"Ushiriki wetu katika Save Soil Walkathon unaonesha dhamira yetu ya kusaidia juhudi za kuongeza uelewa wa jamii na kulinda rasilimali za asili kwa manufaa ya vizazi vijavyo."

"Tutaendelea kushirikiana na Serikali, taasisi na wadau mbalimbali katika kutekeleza miradi na kampeni zinazochochea utunzaji wa mazingira, matumizi bora ya rasilimali za asili na maendeleo endelevu nchini," alisema Esther Msuya.
Save Soil Walkathon imeonesha nguvu ya ushirikiano kati ya Serikali, asasi za kiraia, sekta binafsi na wananchi katika kuendeleza agenda ya utunzaji wa mazingira. Washiriki walihamasishwa kuchukua hatua za vitendo ikiwemo upandaji miti, matumizi bora ya ardhi, uhifadhi wa vyanzo vya maji na ulinzi wa rasilimali za asili kwa ajili ya mustakabali wa taifa.

Wadhamini wa Save Soil Walkathon:
  • GSG Energies
  • META JCB
  • SRL
  • UHAI Pure Drinking Water
  • ISUZU Tanzania

Share:

PROF. NAGU ARIDHISHWA NA HUDUMA ZINAZOTOLEWA BANDA JUMUISHI LA OFISI YA WAZIRI MKUU SABASABA

     

Na. Mwandishi Wetu - Dar es Salaam | Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Afya katika Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Tumaini Nagu, ametembelea Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam, na kupongeza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi.

Akiwa katika ziara hiyo, Prof. Nagu amepata fursa ya kutembelea sehemu mbalimbali za banda hilo na kupokea maelezo kuhusu huduma na mifumo mbalimbali inayowezesha wananchi kupata taarifa na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake.

Amesema banda hilo limekuwa jukwaa muhimu la kuwaelimisha wananchi kuhusu utekelezaji wa programu na miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha utoaji wa huduma za kijamii, hususan katika sekta ya afya, elimu, utawala bora na maendeleo ya serikali za mitaa.

Prof. Nagu amewapongeza watumishi wanaohudumu katika banda hilo kwa kujituma, kutoa elimu kwa ufasaha na kuhakikisha kila mwananchi anayefika anapata huduma na taarifa sahihi zinazomwezesha kufahamu shughuli zinazotekelezwa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu.

Aidha, amewataka kuendelea kutumia maonesho hayo kama fursa ya kusikiliza maoni ya wananchi, kupokea changamoto zao na kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu huduma zinazotolewa, ili kuongeza uelewa na kuimarisha uhusiano kati ya Serikali na wananchi.

"Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu limeendelea kuvutia maelfu ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba, ambapo wamekuwa wakipata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Ofisi hii pamoja na taasisi zake kwa lengo la kuboresha ustawi wa wananchi na kuharakisha maendeleo ya Taifa, hivyo wananchi endeleeni kuitumia fursa ya uwepo wa ofisi hii katika maonesho haya," alisema Dkt. Nagu

Aidha,ametumia nafasi hiyo kuipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na Taasisi nyingine zilizowezesha mafanikio ya maonesho hayo huku akiiasa jamii kuendelea kutembelea banda hilo na kupata elimu.

Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini.

Miongoni mwa Taasisi za Ofisi ya Waziri Mkuu zilizoshiriki ni pamoja na PSSSF, WCF, NSSF, OSHA, NEEC, TNBC, CMA, TACAIDS, DCEA,Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, DART, TARURA, Chuo cha Serikali za Mitaa(LGTI) pamoja na Shirika la Masoko Kariakoo.
Share:

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

Popular Posts

Blog Archive

Labels

Blog Archive

Recent Posts

Label Cloud

BIASHARA (331) BURUDANI (4) KIMATAIFA (10) KITAIFA (129) MICHEZO (41) SIASA (3)

Pages