DP WORLD YALETA MAPINDUZI MAKUBWA YA UTENDAJI KAZI NA UFANISI WA KIHISTORIA KATIKA BANDARI YA DAR ES SALAAM

Kupungua kwa zaidi ya asilimia 90 kwa muda wa upakuaji wa shehena kunadhihirisha mabadiliko ya kiutendaji yaliyofanyika ndani ya miaka miwili ya mageuzi ya uendeshaji.

DAR ES SALAAM, TANZANIA – 7 July 2026: Bandari ya Dar es Salaam imeshuhudia mapinduzi makubwa kiutendaji baada ya kampuni ya DP World kuweka rekodi mpya ya kasi ya kuhudumia meli na kupunguza muda wa kushusha mizigo kwa zaidi ya asilimia 90. Mafanikio haya ni hatua kubwa katika mageuzi ya bandari hiyo tangu kampuni hiyo ianze uendeshaji wake rasmi mnamo Aprili 2024.

Chini ya mkataba wa uendeshaji wa miaka 30, kampuni ya DP World inaendelea kuwekeza katika ukarabati na upanuzi wa bandari hiyo ili kuunga mkono malengo ya muda mrefu ya nchi kiuchumi na kibiashara.

Kupitia uhamishaji wa mifumo ya kisasa ya uendeshaji wa meli za mizigo ya magari (RoRo) unaowezesha bandari kuhudumia meli kubwa na zenye mahitaji ya hali ya juu kwa usalama zaidi, huku ikipunguza gharama za mnyororo wa ugavi, huku ikiongeza ushindani wa kibiashara na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Mageuzi haya yameleta mapinduzi makubwa kwa kupunguza muda wa kushusha mizigo ya aina hiyo kwa zaidi ya asilimia 90—kutoka zaidi ya saa 300 hadi chini ya saa 28. Hatua hii imeweka kiwango kipya kabisa cha ufanisi katika bandari hiyo.
Meli hiyo yenye urefu wa mita 240, ndiyo meli ndefu zaidi kuwahi kutia nanga katika Bandari ya Dar es Salaam, ikiwa na uwezo wa kubeba hadi magari 7,790. Ilitumia muda wa saa 27 tu kukamilisha zoezi la kushusha shehena ya magari 779, ambayo mengi yake yalikuwa ni magari makubwa na mitambo mizito.

Akizungumzia hatua hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa DP World nchini Tanzania, Martin Jacob, alisema: “Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, tumefanya mapinduzi makubwa katika mfumo wa usafirishaji wa shehena kupitia Bandari ya Dar es Salaam. Kasi kubwa ya kuhudumia meli, kuongezeka kwa uwezo wa bandari, na uwezo wa kupokea meli kubwa zaidi zenye mizigo mchanganyiko, kunazidi kuimarisha nafasi ya Tanzania kama lango kuu la biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki, huku kukileta tija kwa wateja, wafanyabiashara na uchumi kwa ujumla.

Mabadiliko kuelekea matumizi ya meli maalum za kusafirisha magari na malori (PCTC), yaliyofanyika kwa ushirikiano na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), yamewezesha ushushaji wa magari na mitambo mizito kwa kasi, usalama na ufanisi mkubwa zaidi. Hatua hii ya kuacha mifumo ya zamani ya upakuaji mizigo ya kawaida imeleta mafanikio endelevu katika makundi yote ya shehena huku yakiimarisha nafasi ya Dar es Salaam kama kitovu cha biashara chenye ushindani mkubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Muhtasari wa Mageuzi na Matokeo
  • Kasi ya kushusha shehena kuongezeka kwa 90% – Muda wa kushusha mizigo ya aina hiyo umepungua kutoka zaidi ya saa 300 hadi chini ya saa 28.
  • Uwekaji wa rekodi mpya ya meli – Kufanikiwa kupokelewa na kuhudumiwa kwa meli ndefu zaidi kuwahi kufika bandarini, yenye urefu wa mita 240.
  • Upanuzi wa uwezo na ufanisi – Kuanza rasmi kwa uendeshaji wa meli maalum za magari (PCTC) kumeongeza kasi na usalama wa kazi.
  • Uchochezi wa ukuaji wa uchumi – Kupungua kwa gharama za usafirishaji kunasaidia kuongeza tija, kukuza Pato la Taifa, na kuleta ushindani wa kibiashara.
  • Kuendeleza wataalamu wazalendo – Zaidi ya Watanzania 2,900 wamepata ajira na wanaendelea kupatiwa mafunzo ya kiutendaji na usalama kazini.
Ili kukidhi ongezeko la shehena na ujio wa meli kubwa zaidi, DP World inaendelea kuwekeza katika kuwajengea uwezo wafanyakazi na kuimarisha usalama bandarini hapo. Kituo hicho kimeajiri zaidi ya Watanzania 2,900, ambao wanapatiwa vyeti vinavyotambulika kimataifa pamoja na mafunzo maalum ya kiutendaji na ukabilianaji wa dharura, kwa lengo la kuhakikisha shughuli za bandari zinakuwa salama, za ufanisi na za kuaminika.

Uwekezaji wetu endelevu katika Bandari ya Dar es Salaam unaonyesha dhamira ya muda mrefu ya DP World katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa Afrika na kuiunganisha na mifumo ya biashara ya kimataifa. Kupitia ushirikiano wetu na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), hatuboreshi tu miundombinu hii muhimu, bali pia tunawezesha mtangamano wa kikanda, kupunguza vikwazo vya kibiashara, na kutengeneza fursa endelevu za kiuchumi," anasema Mohammed Akoojee, Ofisa Mtendaji Mkuu na Mkurugenzi Mkuu wa DP World kanda ya Afrika.
Kwa taarifa zaidi kuhusu jinsi DP World inavyoboresha biashara ya kimataifa, tembelea tovuti yetu: www.dpworld.com

Kwa maswali ya vyombo vya habari, tafadhali wasiliana na;

Keitumetse Masike
Mkurugenzi: Mawasiliano ya Biashara na Mikakati Afrika
Keitumetse.masike@dpworld.com
+27 61 831 8490

Kholiswa Hashe
Meneja Mwandamizi, Mawasiliano – Afrika Mashariki
Kholiswa.Hashe@dpworld.com
+27 72 741 0099

Fuatilia DP World kupitia:



Kuhusu DP World

DP World inabadilisha mustakabali wa biashara ya kimataifa ili kuboresha maisha ya watu kila mahali. Tukifanya kazi katika mabara sita tukiwa na timu ya wafanyakazi zaidi ya 125,000, tunajumuisha miundombinu ya kimataifa na uzoefu wa maeneo husika ili kutoa huduma jumuishi za ugavi. Kuanzia Bandari na Vituo vya Huduma (Terminals) hadi Huduma za Majini, Lojistiki na Teknolojia, tunatumia ubunifu kutengeneza njia bora zaidi za kufanya biashara—huku tukipunguza changamoto kuanzia kiwandani hadi mlangoni mwa mteja.

Katika kanda ya kusini mwa jangwa la Sahara, DP World imeajiri zaidi ya watu 28,000, ina magari zaidi ya 6,300, na inafanya kazi katika masoko 48.
TUNAFANIKISHA MTIRIRIKO WA BIASHARA
Share:

BENKI YA ABSA TANZANIA YATOA SHILINGI MILIONI 20 KUSAIDIA MATIBABU YA WATOTO WENYE MAGONJWA YA MOYO

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto), akizungumza katika hafla ya utiaji saini Hati za Makubaliano (MoU) ya ushirikiano kati ya benki hiyo na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), ambapo pia benki hiyo ilitoa Shilingi Milioni 20 kusaidia matibabu ya watoto wenye changamoto ya magonjwa ya moyo wanaotoka katika familia zenye uhitaji. Hafla hiyo ilifanyika katika taasisi hiyo, jijini Dar es Salaam jana. Kutoka kushoto ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge, Meneja Mkuu wa Taasisi ya Global Medicare, Bw. Daniel Lazaro, na Ofisa Huduma za Sheria wa JKCI, Bi. Ummukulthum Said.

KATIKA kuendeleza juhudi zake za kuchangia ustawi wa jamii kupitia programu zake za uwajibikaji kwa jamii, Benki ya Absa Tanzania imetoa msaada wa Shilingi milioni 20 kwa ajili ya kusaidia matibabu ya watoto wanaoishi na magonjwa ya moyo nchini Tanzania.

Msaada huo umetolewa kupitia Heart Team Africa Foundation (HTAF), taasisi isiyo ya kiserikali iliyoanzishwa na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), yenye lengo la kuwasaidia watoto wanaotoka katika mazingira yenye uhitaji Ili kupata matibabu na huduma za moyo hivyo kuokoa maisha yao.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini wa Hati ya Makubaliano (MoU), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Obedi Laiser, alisema ushirikiano huo unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuwa chachu ya maendeleo mema katika jamii inazozihudumia.

"Dhamira yetu ni kuwa chachu ya maendeleo mema katika kila tunachofanya, na ushirikiano huu ni uthibitisho wa dhamira hiyo kwa vitendo. Tunatambua kazi kubwa inayofanywa na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete katika kutoa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo kwa watoto na familia nchini Tanzania. Kupitia Hati hii ya Makubaliano, tunaongeza fursa kwa watoto wanaoishi na magonjwa ya moyo kupata matibabu yanayookoa maisha na kuzipa matumaini familia zinazokabiliwa na changamoto kubwa za kiafya na kifedha."

"Kila mtoto anastahili nafasi ya kuishi maisha yenye afya na yenye tija. Kwa kuwekeza katika afya zao leo, tunawekeza katika mustakabali wao, ustawi wa familia zao na maendeleo endelevu ya jamii zetu. Tunajivunia kushirikiana na JKCI katika mpango huu muhimu unaolenga kuboresha maisha ya watoto kote nchini Tanzania”, alisema Bw. Laiser.

Akipokea msaada huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge, aliishukuru Benki ya Absa Tanzania kwa mchango huo, akieleza kuwa utasaidia kuongeza upatikanaji wa matibabu muhimu ya moyo kwa watoto wanaoishi na magonjwa ya moyo.

Alisema magonjwa ya moyo yanaongezeka kwa kasi duniani ikiwa ni pamoja na Tanzania, waathirika pia wakiwa ni watoto ambao wengi wao zaidi ya asilimia 70 wanazaliwa wakiwa na changamoto za magonjwa hayo licha ya wale wanaoyapata baada ya kuzaliwa.

"Msaada huu umekuja wakati muhimu kwa watoto wengi na familia zinazohitaji huduma maalumu za matibabu ya moyo," alisema. "Mbali na kutusaidia kuokoa maisha, unadhihirisha nafasi muhimu ya ushirikiano kati ya sekta binafsi na taasisi za afya katika kuimarisha utoaji wa huduma za afya na kuboresha matokeo ya matibabu kwa wagonjwa nchini Tanzania."

Namshukuru Mheshimiwa rais na serikali yake kwa kusaidia zaidi ya asilimia 70 ya gharama, kwa niaba ya bodi ya JKCI, kwa niaba ya serikali kwa jinsi mnavyofanya kumuunga mkono mheshimiwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kurudisha matumaini na kuwapa watu upendo, Absa mmefanya,mmetekeleza kile ambacho rais anakihitaji”, aliongeza Dk. Kisenge.

Nao baadhi ya wazazi wanufaika wa msaada huo, Mariam Athumani ambaye mtoto wake Lightness ameshafanyiwa upasuaji wa moyo na Adam Nuhu ambaye mtoto wake Ajmalbey anayesubiri upasuaji wametoa shukurani kwa Benki ya Absa huku wakiziomba taasisi nyingine kujitolea kuwasaidia kutokana na changamoto kubwa wanazozipata wazazi wenye watoto wenye magonjwa ya moyo.

Benki ya Absa inasema mchango huo unathibitisha dhamira ya benki hiyo ya ‘kuiwezesha Afrika ya kesho, pamoja... Hatua moja baada ya nyingine’, kupitia kusaidia upatikanaji wa matibabu yanayookoa maisha kwa watoto wenye magonjwa ya moyo, ikilenga kuboresha matokeo ya afya, kupunguza mzigo wa kifedha kwa familia zilizoathirika, na kuchangia kujenga jamii zenye afya bora na ustahimilivu zaidi nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge wakisaini Hati za Makubaliano (MoU) ya ushirikiano kati ya pande hizo mbili, katika hafla ambayo pia benki hiyo ilitoa Shilingi Milioni 20 kusaidia matibabu ya watoto wenye changamoto ya magonjwa ya moyo wanaotoka katika familia zenye uhitaji. Hafla hiyo ilifanyika katika taasisi hiyo, jijini Dar es Salaam jana. Kutoka kushoto ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi na Meneja Mkuu wa Taasisi ya Global Medicare, Bw. Daniel Lazaro.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge wakibadilishana Hati za Makubaliano (MoU) ya ushirikiano kati ya pande hizo mbili muda mfupi baada ya kuzisaini katika hafla ambayo pia benki hiyo ilitoa Shilingi Milioni 20 kusaidia matibabu ya watoto wenye changamoto ya magonjwa ya moyo wanaotoka katika familia zenye uhitaji. Hafla hiyo ilifanyika katika taasisi hiyo, jijini Dar es Salaam jana. Kutoka kushoto ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi na Meneja Mkuu wa Taasisi ya Global Medicare, Bw. Daniel Lazaro.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge (wa nne kulia) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kulia kwake), wakipiga picha ya pamoja pamoja na wazazi na watoto wao wanaopatiwa matibabu ya moyo katika taasisi hiyo mara baada ya tukio hilo jijini Dar es Salaam jana.
Share:

BENKI YA ABSA YAENDELEA KUJIZATITI KATIKA KUWAWEZESHA WAJASIRIAMALI NCHINI

Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Victor Nchimbi akizungumza na baadhi ya wajasiriamali kuhusu huduma zinazotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, katika hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.

KATIKA kutambua mchango wa wanawake wajasiriamali katika kuinua Uchumi wa Taifa, Benki ya Absa Tanzania imeendelea kuhamasisha wajasiriamali hao kujiunga na akaunti ya SHE ya benki hiyo ambayo pamoja na faida nyingine, akaunti hiyo haina makato ya mwezi ya kuendesha akaunti, ada za kufanyia miamala na kuweza kufanya miamala kwa kutumia fedha za kitanzania na za kigeni.

Akizungumza wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani, jijini Dar es Salaam hivi karibuni, ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini, Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa benki hiyo, Bw. Victor Nchimbi alisema kwa kupitia akaunti ya SHE, wanajasiriamali wanawake wanapata mafunzo maalumu ya jinsi ya kuendesha biashara zao kwa mafanikio.

Tukiwa kama wadau wakubwa wa sekta hii ya ujasiriamali na kwa kutambua mchango wa wajasiamali Tanzania tumekuwa na huduma mbalimbali tunazowapatia wajasiriamli wetu, ikiwa ni pamoja na mikopo yenye gharama nafuu, huduma za kidigitali, ukiangalia katika maadhimisho haya, waadhimishaji wengi ni wanawake, tunayo akaunti ya SHE, iliyojikita katika kuwawezesha wanawake kuichumi”, alisema.

Akizungumza katika hafla hiyo, mmoja wa wajasiriamali anayejishughulisha na biashara ya vipodozi, Bi. Maua Jumanne alisema, suala la elimu ya mitaji, mikopo na jinsi ya kufanya biashara kwa ufanisi limekuwa ni changamoto kwa wanawake wajasiriamali wengi, hivyo akatoa ushauri kwa benki mbalimbali kuyapa uzito mambo hayo.

Natoa ushauri kwa watu wa mabenki kutufikia na kutupa elimu ya mitaji na mikopo ya kutusaidia sisi wajasiriamali wadogo tuweze kukua katika biashara zetu, na kuepukana na mikopo inayotolewa na vikundi vya watoa mikopo vya kausha damu”, alisema Bi. Maua.

Benki ya Absa imeendelea kujitolea katika kuunda majukwaa yanayofikika kwa urahisi ambapo Biashara Ndogo, Ndogo za Kati na za Kati, zinaweza kubadilishana mbinu bora za biashara, kupata fursa za ufadhili, na kuhamasisha ubunifu, huku ikidumisha lengo kuu la benki hiyo la 'Kuiwezesha Afrika ya kesho, pamoja, hatua moja baada ya jingine'.
Meneja Bidhaa wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa (kulia) akizungumza kuhusu huduma zizotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, kwa baadhi ya wahudhuriaji waliofika katika banda lao, katika Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.
Ofisa Huduma kwa Wateja wa Benki ya Absa, Bi. Mboni Sabura (katikati) akizungumza na baadhi ya wajasiriamali kuhusu huduma zinazotolewa na benki hiyo hususani akaunti maalumu ya wanawake ya She, katika hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini, jijini Dar es Salaam hivi karibuni.Kulia ni Meneja Bidhaa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.
Meneja Bidhaa wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa (kulia) akizungumza kuhusu huduma zizotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, kwa baadhi ya wajasiriamali waliofika katika Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani, ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kuwezesha tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.
Baadhi ya wawezeshaji na wajasiriamali waliojitoleza kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani wakipiga picha ya pamoja mara baada ya kukamilika kwa tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Benki ya Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini hafla hiyo. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.
Share:

OWM YASISITIZA UJUMUISHWAJI WA WATU WENYE ULEMAVU KATIKA MIPANGO YA TAIFA

Na Mwandishi Wetu – Dar es Salaam | SERIKALI imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha Watu Wenye Ulemavu wanapata nafasi sawa katika nyanja zote za maendeleo, ikiwa ni pamoja na kijamii, kiuchumi na kisiasa, kupitia sera, sheria na mipango jumuishi inayotekelezwa nchini.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt. Jim Yonazi wakati wa ufunguzi wa kikao kazi kilichowakutanisha viongozi wa vyama vya Watu Wenye Ulemavu na mashirika yasiyo ya kiserikali kujadili utekelezaji wa sera, sheria na miongozo ya ujumuishaji nchini.
Amesema hatua kubwa zimeendelea kuchukuliwa katika kuhakikisha hakuna mwananchi anayeachwa nyuma, ambapo Sera ya Taifa ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2004 pamoja na Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 zimekuwa msingi muhimu wa utekelezaji wa haki na usawa kwa kundi hilo.

Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa kila sera, mpango na huduma inayotekelezwa nchini inazingatia ujumuishaji wa Watu Wenye Ulemavu tangu hatua ya upangaji, utekelezaji, ufuatiliaji hadi tathmini, ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma,” amesema Dkt. Jim Yonazi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa mawasiliano bora na uratibu imara kati ya Serikali, vyama vya Watu Wenye Ulemavu na mashirika yasiyo ya kiserikali, akibainisha kuwa ushirikiano huo ni msingi muhimu wa kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa shughuli za maendeleo.
Amesema ujumuishaji si jukumu la sekta moja pekee, bali ni wajibu wa kila taasisi, kila sekta na kila mdau wa maendeleo. “Tunapaswa kufanya kazi kwa pamoja ili kuhakikisha huduma zote zinamfikia kila mwananchi kwa usawa,” alisisitiza.

Dkt. Yonazi pia ametoa wito wa kuimarishwa kwa mifumo ya mawasiliano inayowezesha Watu Wenye Ulemavu kupata taarifa kwa urahisi, ikiwemo matumizi ya lugha ya alama, maandishi ya Breli, teknolojia saidizi na mifumo mingine jumuishi.

Serikali inatambua mchango mkubwa unaotolewa na vyama vya Watu Wenye Ulemavu pamoja na mashirika yasiyo ya kiserikali katika kutoa huduma za utetezi wa haki, elimu kwa umma, mafunzo ya kujenga uwezo, uwezeshaji kiuchumi, huduma za afya, elimu jumuishi na ushauri wa kitaalamu,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Yonazi amesema kuwa pamoja na jitihada ambazo Serikali imeendelea kuzichukua, bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazohitaji ushirikiano wa wadau wote.
Amesema changamoto hizo ni pamoja na uelewa usioridhisha kuhusu masuala ya ujumuishaji katika baadhi ya sekta, utekelezaji usiofanana wa sera na sheria, pamoja na changamoto za upatikanaji wa huduma jumuishi zinazokidhi mahitaji ya Watu Wenye Ulemavu.

Kutokana na hali hiyo, kikao hiki ni muhimu sana kwa kuwa kinatoa fursa ya kujadili kwa kina namna bora ya kuimarisha ujumuishaji wa huduma katika sekta zote.

Awali, Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA), Bi. Tungi Mwanjala, ameiomba Serikali kuendelea kuangalia uwezekano wa kuwatambua watoto wa wazazi wenye ulemavu ili waweze kunufaika na fursa mbalimbali za maendeleo, ikiwemo kupata mikopo ya elimu ya juu kwa urahisi.
Bi.Mwanjala ameeleza kuwa, Serikali imepiga hatua kubwa kwa kukamilisha muongozo na mfumo wa utambuzi wa watu wenye ulemavu, lakini bado kuna haja ya kupanua utambuzi huo kwa watoto wa wazazi wenye ulemavu.

"Tunashukuru Serikali kwa kukamilisha muongozo na mfumo wa kutambua watu wenye ulemavu. Hata hivyo, tunaomba pia watoto wetu watambuliwe kupitia mfumo maalumu utakaowezesha kupata vitambulisho, jambo litakalowarahisishia kupata mikopo ya elimu ya juu na fursa nyingine za maendeleo ikiwamo ajira kwa kuzingatia utaratibu uliopo," amesema.
Share:

RAIS DKT. MWINYI: TAASISI ZA KIFEDHA ZA NDANI ZINAFAA KUIMARISHA USHIRIKIANO NA SERIKALI KATIKA MIRADI YA MAENDELEO

  

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akimkabidhi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia), tuzo ya kumbukumbu kama ishara ya kuthamini ushirikiano imara kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta ya fesha pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi visiwani humo. Ilikuwa wakati wa ziara ya Mkurugenzi huyo pamoja na ujumbe wake, Ikulu, mjini Zanzibar, juzi.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesisitiza kuwa bado kuna fursa nyingi kwa taasisi za kifedha za ndani kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Rais Dkt. Mwinyi alitoa kauli hiyo jana alipokutana na ujumbe wa Absa Bank Tanzania, ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw. Obeid Laiser, aliyefanya ziara ya heshima Ikulu Zanzibar.

Amesema Serikali iko tayari kushirikiana kwa karibu na benki za ndani zinazodhihirisha dhamira ya kusaidia jitihada za maendeleo, hususan katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya kiuchumi na kijamii katika sekta mbalimbali.

Rais Dkt. Mwinyi aliipongeza Absa Bank Tanzania kwa utayari wake wa kushirikiana na Serikali na kuchangia maendeleo ya Zanzibar. Aidha, alieleza kuwa Serikali imeimarisha mifumo ya kufadhili miradi ya maendeleo kwa kupanua vyanzo vya fedha nje ya bajeti ya kawaida, hatua inayolenga kuharakisha utekelezaji wa miradi na kuongeza ufanisi.

Rais aliwahakikishia viongozi wa benki hiyo kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za kifedha katika kurahisisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo kupitia mikopo na mipango mingine ya kifedha.

Kwa upande wake, Bw. Obeid Laiser alishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ushirikiano wake wa kudumu na benki hiyo na kumpongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa uongozi wake uliosababisha maendeleo makubwa Zanzibar. Alisisitiza tena dhamira ya Absa Bank Tanzania kuendeleza ushirikiano na Serikali katika kusaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi na uchumi wa Zanzibar.

Bw. Laiser pia alieleza mchango wa Absa katika uchumi wa Zanzibar, akibainisha ueneaji na athari zake kupitia utoaji wa huduma za kifedha kwa watu binafsi, wafanyabiashara na mashirika makubwa.

Katika taarifa iliyotolewa baada ya mkutano huo, Bw. Laiser alieleza shukrani za benki kwa Serikali ya Zanzibar kwa kuunda mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji.

Tunajivunia kupata fursa ya kukutana na Mheshimiwa Rais Hussein Ali Mwinyi na kujadili safari ya maendeleo ya kipekee ya Zanzibar. Kama mshirika wa kifedha anayeaminika, Absa itaendelea kujitolea kusaidia matarajio ya wananchi wa Zanzibar kupitia upatikanaji wa fedha, urahisishaji wa uwekezaji, ukuzaji wa ujasiriamali na suluhisho bunifu za kibenki zinazochangia katika ukuaji endelevu wa uchumi.

Absa inahudumia zaidi ya wateja 11,000 Zanzibar, inasimamia amana zinazozidi TZS bilioni 136 na imekopesha zaidi ya TZS bilioni 64 kwa watu binafsi, biashara ndogo na za kati pamoja na makampuni makubwa yanayofanya kazi katika sekta kuu za uchumi ikiwemo utalii, hoteli, biashara na uchuuzi,” alisema Bw. Laiser.

Bw. Laiser pia alisisitiza mchango wa Absa nje ya huduma za kibenki kupitia miradi ya uwajibikaji wa kijamii, ikiwemo kusaidia afya ya mama na mtoto chini ya mpango wa Uzazi ni Maisha, unaotekelezwa kwa ushirikiano na AMREF Health Africa na Wizara ya Afya Zanzibar. Kupitia mpango huu, Absa imechangia kuboresha upatikanaji wa vifaa muhimu vya kitabibu na kuimarisha huduma salama za kujifungua kwa akina mama na watoto wachanga Zanzibar.

Absa Bank Tanzania itaendelea kujitolea kwa dhima yake ya 'Kuiwezesha Afrika ya kesho pamoja… hatua moja baada ya nyingine' na kusaidia ustawi wa muda mrefu na mafanikio ya wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akizungumza na ujumbe kutoka Benki ya Absa Tanzania, ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw, Obedi Laiser (wa tano kushoto), ulipomtembelea Ikulu, Zanzibar juzi. Bw. Laiser alitoa shukurani za benki kutokana na ushirkiano uliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta za kibenki nchini pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi yanayofanyika visiwani humo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (Katikati), akipiga picha ya kumbukumbu na ujumbe kutoka Benki ya Absa Tanzania, ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw, Obedi Laiser (kulia kwake), ulipomtembelea Ikulu, Zanzibar juzi. Wakati wa mazungumzo yao, Bw. Laiser alitoa shukurani za benki kutokana na ushirkiano uliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta za kibenki nchini pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi yanayofanyika visiwani humo. (PICHA NA IKULU)
Share:

DCB YAZINDUA KAMPENI YA "TUMA BURE, SHINDA KILA WIKI" KUVUTIA WATEJA WA HUDUMA ZA KIDIJITALI

 

DAR ES SALAAM: Benki ya DCB imezindua kampeni maalum ya miezi sita ijulikanayo kama "Tuma Bure, Shinda Kila Wiki", inayolenga kuhamasisha matumizi ya huduma za kidijitali na kuongeza ujumuishaji wa huduma za kifedha nchini kwa kuwapatia wateja nafasi ya kushinda zawadi mbalimbali huku wakifanya miamala bila kutozwa gharama.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya DCB, Sabasaba Moshingi, amesema benki hiyo imefanya maboresho makubwa ya huduma zake za kidijitali baada ya kubaini kuwa wateja wengi wanahitaji huduma za haraka, salama, nafuu na zinazopatikana muda wote. Amesema kupitia mfumo mpya wa DCB Pesa App, wateja wanaweza kufungua akaunti popote walipo nchini na kufanya miamala mbalimbali bila makato.
Moshingi amesema kampeni hiyo pia inalenga kuunga mkono juhudi za Serikali za kuongeza ushiriki wa wananchi katika huduma rasmi za kifedha, huku akiwahimiza Watanzania kutumia huduma za benki ili kukuza biashara zao na kufikia malengo ya kiuchumi kwa urahisi zaidi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko wa DCB, Geofrey Magugi, amesema mteja anayefungua akaunti kupitia DCB Pesa App na kufanya angalau muamala mmoja ataingia kwenye droo ya kila wiki yenye zawadi ya Shilingi 100,000 kwa washindi 10,amesema wateja watakaofanya miamala zaidi ya mitatu kwa mwezi watapata nafasi ya kushinda zawadi kubwa zaidi ikiwemo Shilingi milioni moja kila mwezi.

Naye Mkurugenzi wa Biashara wa DCB, Ramadhani Mganga, amesema kampeni hiyo itadumu hadi Desemba mwaka huu na inalenga kuwazawadia wateja wanaotumia huduma za benki kwa njia za kidijitali, amesema DCB imeendelea kuwa miongoni mwa taasisi za fedha zinazoweka kipaumbele katika ubunifu wa huduma nafuu, huku ikitoa fursa kwa Watanzania kufungua akaunti na kufanya miamala kutoka mahali popote nchini bila kulazimika kutembelea matawi ya benki.
Mganga amesema pamoja na faida ya kutuma fedha bila makato, wateja watakaoshiriki kampeni hiyo watakuwa na nafasi ya kushinda zawadi za kila wiki, kila mwezi na zawadi kubwa itakayotolewa mwishoni mwa kampeni mwezi Desemba, akiwataka Watanzania kuchangamkia fursa hiyo kwa kufungua akaunti za DCB na kutumia huduma zake za kidijitali.
Share:

BENKI YA ABSA YAUNGANA NA TPSF KUWANOA WAJASIRIAMALI WANAWAKE

Meneja Miradi wa Benki ya Absa, Bi. Munira Chambuso akizungumza katika semina iliyoandaliwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, ikihuhusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.

DAR ES SALAAM | Wanawake wafanyabiashara kutoka sekta mbalimbali nchini wamehimizwa kuendelea kujengewa uwezo wa elimu ya fedha ili kuwawezesha kufanya maamuzi sahihi ya kifedha, kukuza biashara zao na kuongeza mchango wao katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa na Meneja wa Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi, wakati wa mafunzo ya elimu ya fedha yaliyoandaliwa kwa ushirikiano kati ya Benki ya Absa Tanzania na Shirikisho la Sekta Binafsi Tanzania (TPSF).

Akizungumza katika mafunzo hayo, Bi. Lukuvi amesema mpango huo ulianza mwaka jana kama sehemu ya ajenda ya uwajibikaji kwa jamii ya benki hiyo, inayolenga kuwawezesha wananchi, hususan wanawake wajasiriamali, kupata maarifa ya kifedha yatakayowasaidia kuwekeza kwa ufanisi na kuimarisha biashara zao.

Amesema mafunzo hayo yamewakutanisha wanawake wamiliki wa biashara kutoka sekta mbalimbali kwa lengo la kuwapa elimu kuhusu usimamizi wa fedha, uwekezaji na mikakati ya kuongeza mapato pamoja na kukuza biashara zao kwa njia endelevu.

Tunafurahi kuona wanawake wengi wakishiriki mafunzo haya. Tunaamini elimu ya fedha ni nyenzo muhimu katika kuwajengea uwezo wa kufikia mafanikio ya kiuchumi na kuimarisha ustawi wa biashara zao,” amesema Bi. Lukuvi.

Aidha, ameishukuru TPSF kwa ushirikiano wake katika kufanikisha mafunzo hayo na kubainisha kuwa ushirikiano huo utaendelea ili kuwafikia wanawake wengi zaidi na kuwapa fursa ya kupata elimu ya fedha na uwekezaji.

Mafunzo hayo yamewaleta pamoja wanawake kutoka sekta mbalimbali ikiwemo biashara, viwanda vidogo, madini, utalii, sekta za ubunifu na ukandarasi, wakiwakilisha wanachama wa TPSF.

Katika mafunzo hayo, wataalamu wa Absa walitoa elimu kuhusu usimamizi wa fedha ikijumuisha masuala ya bajeti, akiba na uwekezaji kwa lengo la kusaidia wajasiriamali kukuza biashara zao na kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kiuchumi.

Kwa upande wake, mwakilishi wa TPSF, Kinanasi Seif, amesema shirikisho hilo litaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuwawezesha wanawake wajasiriamali kupitia programu za mafunzo na elimu zinazolenga kukuza biashara na kuimarisha uchumi wao.

Amesema TPSF imekuwa ikitekeleza programu mbalimbali za kuwawezesha wanawake katika nyanja tofauti za biashara huku ikitambua mchango mkubwa wa wanawake katika maendeleo ya sekta binafsi na uchumi wa taifa kwa ujumla.

Tumefanikiwa kuwaleta pamoja wanawake wajasiriamali kutoka vyama mbalimbali ili wapate mafunzo ya elimu ya fedha na uwekezaji kutoka Benki ya Absa. Tunaamini maarifa haya yatawasaidia kufanya maamuzi sahihi ya kifedha na kukuza biashara zao,” amesema Seif.

Ameongeza kuwa ushirikiano kati ya TPSF na Benki ya Absa ni hatua muhimu katika kuhakikisha wanawake wanapata fursa za kujengewa uwezo na kufikia maendeleo endelevu katika shughuli zao za kiuchumi.

Wakati huo huo, wataalamu kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) walitoa elimu kuhusu utii wa kodi kwa biashara ndogo na za kati (SMEs), wakisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria za kodi katika kujenga biashara imara na endelevu.

Akizungumza katika semina hiyo, Afisa wa TRA, Zephaniah Usange Jamange, amesema kuwa pamoja na walipakodi kutekeleza wajibu wao wa kulipa kodi, ni muhimu pia kufahamu haki zao wanazostahili kupata kutoka kwa mamlaka hiyo.

Amesema miongoni mwa haki hizo ni usiri wa taarifa za kikodi, ambapo taarifa zote zinazowasilishwa na mlipakodi zinapaswa kubaki siri na haziwezi kutolewa kwa watu wasiohusika. Aidha, walipakodi wote wanapaswa kuhudumiwa kwa usawa bila upendeleo wowote.

Walipakodi pia wana haki ya kupinga maamuzi yanayotolewa na maafisa wa kodi pale wanapoona hawajaridhika nayo. Maamuzi ya awali si ya mwisho, hivyo kuna fursa ya kukata rufaa kwa kufuata taratibu zilizowekwa,” amesema Jamange.

Kwa upande wa wajibu, TRA imewakumbusha wafanyabiashara kuhakikisha wanajisajili kwa TIN ndani ya siku tano tangu waanze biashara. Pia wafanyabiashara wanaofikia mauzo yanayostahili kwa mujibu wa sheria wanapaswa kutumia mashine za kutolea risiti za kielektroniki (EFD) na kujisajili kwa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) pale inapohitajika.

Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za pamoja za kukuza ushiriki wa wanawake katika shughuli za kiuchumi kwa kuwapatia ujuzi wa usimamizi wa fedha, uwekezaji, utii wa kodi na uendeshaji bora wa biashara, hatua inayotarajiwa kuchochea ukuaji wa biashara zao na maendeleo ya uchumi wa taifa.
Meneja wa Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (wa pili kutoka kushoto), akizungumza na baadhi ya washiriki, katika semina iliyoandaliwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati ikihusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.
Mkurugenzi wa Wanachama wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Bi. Kinanasy Seif akizngumza katika semina iliyoandaliwa na Benki ya Absa Tanzania kwa kushirikiana na taasisi hiyo kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, ikihusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.
Meneja Bidhaa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa, akizungumza katika semina iliyoandaliwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, Ikihusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.
Ofisa Elimu kwa Mlipa Kodi na Mawasiliano wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Zephania Mange, akitoa elimu kuhusu wajibu wa mlipa kodi katika semina iliyoandaliwa na Benki ya Absa Tanzania kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, Ikihusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.
Wawakilishi kutoka Benki ya Absa na TPSF, wakipiga picha ya kumbukumbu pamoja na washiriki wa semina hiyo pamoja na wawezeshaji wengine, mara baada ya kumalizika kwa semina hiyo, jijini Dar es Salaam jana.
Share:

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

Popular Posts

Blog Archive

Labels

Blog Archive

Recent Posts

Label Cloud

BIASHARA (329) BURUDANI (4) KIMATAIFA (10) KITAIFA (127) MICHEZO (41) SIASA (3)

Pages