
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, ameongoza mamia ya wananchi na wadau mbalimbali wa mazingira katika matembezi ya Save Soil Walkathon, huku akitoa wito kwa Watanzania kushiriki kikamilifu katika juhudi za kulinda udongo na mazingira kwa ajili ya maendeleo endelevu ya taifa.
Mhe. Masauni, ambaye alikuwa mgeni rasmi wa tukio hilo, alishiriki matembezi hayo yaliyoandaliwa na Lions Club of Dar es Salaam Mazingira chini ya kaulimbiu ya “Save Soil, Save Our Future” (Linda Udongo, Linda Mustakabali Wetu).

Tukio hilo liliwakutanisha wadau wa mazingira, taasisi mbalimbali, sekta binafsi na wananchi katika kampeni ya kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kuhifadhi afya ya udongo na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.
Akizungumza baada ya matembezi hayo, Mhe. Masauni alisema afya ya udongo ni msingi wa usalama wa chakula, uhifadhi wa mazingira na ustawi wa uchumi wa taifa, hivyo kuna umuhimu wa kila Mtanzania kushiriki katika juhudi za kuutunza.
"Udongo ni rasilimali muhimu inayobeba maisha yetu ya kila siku. Bila udongo wenye afya hatuwezi kuwa na usalama wa chakula, mazingira bora wala maendeleo endelevu. Ni wajibu wa kila Mtanzania kushiriki katika juhudi za kulinda mazingira na kutumia ardhi kwa njia zinazohifadhi uhai wake kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho," alisema Mhe. Masauni.
Katika kuonesha kwa vitendo dhamira ya kulinda mazingira, Mhe. Masauni pia alipanda mti ikiwa ni ishara ya kujitolea katika uhifadhi wa udongo na mazingira pamoja na kuhamasisha wananchi kushiriki katika upandaji miti kama sehemu ya juhudi za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa ardhi.

Kwa upande wake, Rais wa Lions Club of Dar es Salaam Mazingira, Lion Ramadevi, alisema Save Soil Walkathon ni sehemu ya kampeni pana inayolenga kuhamasisha jamii kutambua mchango mkubwa wa udongo katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kimazi-ngira.
"Save Soil Walkathon si matembezi pekee, bali ni harakati ya kuhamasisha mabadiliko ya tabia na kuwajengea wananchi uelewa wa umuhimu wa kulinda udongo. Tunataka kuona jamii, taasisi na sekta binafsi zikichukua hatua za pamoja katika kuhifadhi mazingira kwa mustakabali wa taifa letu," alisema Lion Ramadevi.
Naye Esther Msuya, Meneja wa Afya, Usalama, Ulinzi na Mazingira (HSSE) wa GSG Energies, alisema kampuni hiyo itaendelea kuunga mkono mipango na kampeni zinazolenga uhifadhi wa mazingira na maendeleo endelevu nchini.
"Kulinda mazingira ni jukumu la kila mmoja wetu. GSG Energies tunaamini kuwa maendeleo ya kweli lazima yaende sambamba na uhifadhi wa mazingira."
"Ushiriki wetu katika Save Soil Walkathon unaonesha dhamira yetu ya kusaidia juhudi za kuongeza uelewa wa jamii na kulinda rasilimali za asili kwa manufaa ya vizazi vijavyo."
"Tutaendelea kushirikiana na Serikali, taasisi na wadau mbalimbali katika kutekeleza miradi na kampeni zinazochochea utunzaji wa mazingira, matumizi bora ya rasilimali za asili na maendeleo endelevu nchini," alisema Esther Msuya.

Save Soil Walkathon imeonesha nguvu ya ushirikiano kati ya Serikali, asasi za kiraia, sekta binafsi na wananchi katika kuendeleza agenda ya utunzaji wa mazingira. Washiriki walihamasishwa kuchukua hatua za vitendo ikiwemo upandaji miti, matumizi bora ya ardhi, uhifadhi wa vyanzo vya maji na ulinzi wa rasilimali za asili kwa ajili ya mustakabali wa taifa.
Wadhamini wa Save Soil Walkathon:

























.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)


















