WAZIRI MASAUNI AONGOZA SAVE SOIL WALKATHON, ATOA WITO WA KULINDA UDONGO NA MAZINGIRA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, ameongoza mamia ya wananchi na wadau mbalimbali wa mazingira katika matembezi ya Save Soil Walkathon, huku akitoa wito kwa Watanzania kushiriki kikamilifu katika juhudi za kulinda udongo na mazingira kwa ajili ya maendeleo endelevu ya taifa.

Mhe. Masauni, ambaye alikuwa mgeni rasmi wa tukio hilo, alishiriki matembezi hayo yaliyoandaliwa na Lions Club of Dar es Salaam Mazingira chini ya kaulimbiu ya “Save Soil, Save Our Future” (Linda Udongo, Linda Mustakabali Wetu).
Tukio hilo liliwakutanisha wadau wa mazingira, taasisi mbalimbali, sekta binafsi na wananchi katika kampeni ya kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kuhifadhi afya ya udongo na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.

Akizungumza baada ya matembezi hayo, Mhe. Masauni alisema afya ya udongo ni msingi wa usalama wa chakula, uhifadhi wa mazingira na ustawi wa uchumi wa taifa, hivyo kuna umuhimu wa kila Mtanzania kushiriki katika juhudi za kuutunza.

"Udongo ni rasilimali muhimu inayobeba maisha yetu ya kila siku. Bila udongo wenye afya hatuwezi kuwa na usalama wa chakula, mazingira bora wala maendeleo endelevu. Ni wajibu wa kila Mtanzania kushiriki katika juhudi za kulinda mazingira na kutumia ardhi kwa njia zinazohifadhi uhai wake kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho," alisema Mhe. Masauni.

Katika kuonesha kwa vitendo dhamira ya kulinda mazingira, Mhe. Masauni pia alipanda mti ikiwa ni ishara ya kujitolea katika uhifadhi wa udongo na mazingira pamoja na kuhamasisha wananchi kushiriki katika upandaji miti kama sehemu ya juhudi za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa ardhi.
Kwa upande wake, Rais wa Lions Club of Dar es Salaam Mazingira, Lion Ramadevi, alisema Save Soil Walkathon ni sehemu ya kampeni pana inayolenga kuhamasisha jamii kutambua mchango mkubwa wa udongo katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kimazi-ngira.

"Save Soil Walkathon si matembezi pekee, bali ni harakati ya kuhamasisha mabadiliko ya tabia na kuwajengea wananchi uelewa wa umuhimu wa kulinda udongo. Tunataka kuona jamii, taasisi na sekta binafsi zikichukua hatua za pamoja katika kuhifadhi mazingira kwa mustakabali wa taifa letu," alisema Lion Ramadevi.

Naye Esther Msuya, Meneja wa Afya, Usalama, Ulinzi na Mazingira (HSSE) wa GSG Energies, alisema kampuni hiyo itaendelea kuunga mkono mipango na kampeni zinazolenga uhifadhi wa mazingira na maendeleo endelevu nchini.

"Kulinda mazingira ni jukumu la kila mmoja wetu. GSG Energies tunaamini kuwa maendeleo ya kweli lazima yaende sambamba na uhifadhi wa mazingira."

"Ushiriki wetu katika Save Soil Walkathon unaonesha dhamira yetu ya kusaidia juhudi za kuongeza uelewa wa jamii na kulinda rasilimali za asili kwa manufaa ya vizazi vijavyo."

"Tutaendelea kushirikiana na Serikali, taasisi na wadau mbalimbali katika kutekeleza miradi na kampeni zinazochochea utunzaji wa mazingira, matumizi bora ya rasilimali za asili na maendeleo endelevu nchini," alisema Esther Msuya.
Save Soil Walkathon imeonesha nguvu ya ushirikiano kati ya Serikali, asasi za kiraia, sekta binafsi na wananchi katika kuendeleza agenda ya utunzaji wa mazingira. Washiriki walihamasishwa kuchukua hatua za vitendo ikiwemo upandaji miti, matumizi bora ya ardhi, uhifadhi wa vyanzo vya maji na ulinzi wa rasilimali za asili kwa ajili ya mustakabali wa taifa.

Wadhamini wa Save Soil Walkathon:
  • GSG Energies
  • META JCB
  • SRL
  • UHAI Pure Drinking Water
  • ISUZU Tanzania

Share:

PROF. NAGU ARIDHISHWA NA HUDUMA ZINAZOTOLEWA BANDA JUMUISHI LA OFISI YA WAZIRI MKUU SABASABA

     

Na. Mwandishi Wetu - Dar es Salaam | Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Afya katika Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Tumaini Nagu, ametembelea Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam, na kupongeza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi.

Akiwa katika ziara hiyo, Prof. Nagu amepata fursa ya kutembelea sehemu mbalimbali za banda hilo na kupokea maelezo kuhusu huduma na mifumo mbalimbali inayowezesha wananchi kupata taarifa na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake.

Amesema banda hilo limekuwa jukwaa muhimu la kuwaelimisha wananchi kuhusu utekelezaji wa programu na miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha utoaji wa huduma za kijamii, hususan katika sekta ya afya, elimu, utawala bora na maendeleo ya serikali za mitaa.

Prof. Nagu amewapongeza watumishi wanaohudumu katika banda hilo kwa kujituma, kutoa elimu kwa ufasaha na kuhakikisha kila mwananchi anayefika anapata huduma na taarifa sahihi zinazomwezesha kufahamu shughuli zinazotekelezwa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu.

Aidha, amewataka kuendelea kutumia maonesho hayo kama fursa ya kusikiliza maoni ya wananchi, kupokea changamoto zao na kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu huduma zinazotolewa, ili kuongeza uelewa na kuimarisha uhusiano kati ya Serikali na wananchi.

"Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu limeendelea kuvutia maelfu ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba, ambapo wamekuwa wakipata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Ofisi hii pamoja na taasisi zake kwa lengo la kuboresha ustawi wa wananchi na kuharakisha maendeleo ya Taifa, hivyo wananchi endeleeni kuitumia fursa ya uwepo wa ofisi hii katika maonesho haya," alisema Dkt. Nagu

Aidha,ametumia nafasi hiyo kuipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na Taasisi nyingine zilizowezesha mafanikio ya maonesho hayo huku akiiasa jamii kuendelea kutembelea banda hilo na kupata elimu.

Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini.

Miongoni mwa Taasisi za Ofisi ya Waziri Mkuu zilizoshiriki ni pamoja na PSSSF, WCF, NSSF, OSHA, NEEC, TNBC, CMA, TACAIDS, DCEA,Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, DART, TARURA, Chuo cha Serikali za Mitaa(LGTI) pamoja na Shirika la Masoko Kariakoo.
Share:

DP WORLD YALETA MAPINDUZI MAKUBWA YA UTENDAJI KAZI NA UFANISI WA KIHISTORIA KATIKA BANDARI YA DAR ES SALAAM

Kupungua kwa zaidi ya asilimia 90 kwa muda wa upakuaji wa shehena kunadhihirisha mabadiliko ya kiutendaji yaliyofanyika ndani ya miaka miwili ya mageuzi ya uendeshaji.

DAR ES SALAAM, TANZANIA – 7 July 2026: Bandari ya Dar es Salaam imeshuhudia mapinduzi makubwa kiutendaji baada ya kampuni ya DP World kuweka rekodi mpya ya kasi ya kuhudumia meli na kupunguza muda wa kushusha mizigo kwa zaidi ya asilimia 90. Mafanikio haya ni hatua kubwa katika mageuzi ya bandari hiyo tangu kampuni hiyo ianze uendeshaji wake rasmi mnamo Aprili 2024.

Chini ya mkataba wa uendeshaji wa miaka 30, kampuni ya DP World inaendelea kuwekeza katika ukarabati na upanuzi wa bandari hiyo ili kuunga mkono malengo ya muda mrefu ya nchi kiuchumi na kibiashara.

Kupitia uhamishaji wa mifumo ya kisasa ya uendeshaji wa meli za mizigo ya magari (RoRo) unaowezesha bandari kuhudumia meli kubwa na zenye mahitaji ya hali ya juu kwa usalama zaidi, huku ikipunguza gharama za mnyororo wa ugavi, huku ikiongeza ushindani wa kibiashara na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Mageuzi haya yameleta mapinduzi makubwa kwa kupunguza muda wa kushusha mizigo ya aina hiyo kwa zaidi ya asilimia 90—kutoka zaidi ya saa 300 hadi chini ya saa 28. Hatua hii imeweka kiwango kipya kabisa cha ufanisi katika bandari hiyo.
Meli hiyo yenye urefu wa mita 240, ndiyo meli ndefu zaidi kuwahi kutia nanga katika Bandari ya Dar es Salaam, ikiwa na uwezo wa kubeba hadi magari 7,790. Ilitumia muda wa saa 27 tu kukamilisha zoezi la kushusha shehena ya magari 779, ambayo mengi yake yalikuwa ni magari makubwa na mitambo mizito.

Akizungumzia hatua hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa DP World nchini Tanzania, Martin Jacob, alisema: “Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, tumefanya mapinduzi makubwa katika mfumo wa usafirishaji wa shehena kupitia Bandari ya Dar es Salaam. Kasi kubwa ya kuhudumia meli, kuongezeka kwa uwezo wa bandari, na uwezo wa kupokea meli kubwa zaidi zenye mizigo mchanganyiko, kunazidi kuimarisha nafasi ya Tanzania kama lango kuu la biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki, huku kukileta tija kwa wateja, wafanyabiashara na uchumi kwa ujumla.

Mabadiliko kuelekea matumizi ya meli maalum za kusafirisha magari na malori (PCTC), yaliyofanyika kwa ushirikiano na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), yamewezesha ushushaji wa magari na mitambo mizito kwa kasi, usalama na ufanisi mkubwa zaidi. Hatua hii ya kuacha mifumo ya zamani ya upakuaji mizigo ya kawaida imeleta mafanikio endelevu katika makundi yote ya shehena huku yakiimarisha nafasi ya Dar es Salaam kama kitovu cha biashara chenye ushindani mkubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Muhtasari wa Mageuzi na Matokeo
  • Kasi ya kushusha shehena kuongezeka kwa 90% – Muda wa kushusha mizigo ya aina hiyo umepungua kutoka zaidi ya saa 300 hadi chini ya saa 28.
  • Uwekaji wa rekodi mpya ya meli – Kufanikiwa kupokelewa na kuhudumiwa kwa meli ndefu zaidi kuwahi kufika bandarini, yenye urefu wa mita 240.
  • Upanuzi wa uwezo na ufanisi – Kuanza rasmi kwa uendeshaji wa meli maalum za magari (PCTC) kumeongeza kasi na usalama wa kazi.
  • Uchochezi wa ukuaji wa uchumi – Kupungua kwa gharama za usafirishaji kunasaidia kuongeza tija, kukuza Pato la Taifa, na kuleta ushindani wa kibiashara.
  • Kuendeleza wataalamu wazalendo – Zaidi ya Watanzania 2,900 wamepata ajira na wanaendelea kupatiwa mafunzo ya kiutendaji na usalama kazini.
Ili kukidhi ongezeko la shehena na ujio wa meli kubwa zaidi, DP World inaendelea kuwekeza katika kuwajengea uwezo wafanyakazi na kuimarisha usalama bandarini hapo. Kituo hicho kimeajiri zaidi ya Watanzania 2,900, ambao wanapatiwa vyeti vinavyotambulika kimataifa pamoja na mafunzo maalum ya kiutendaji na ukabilianaji wa dharura, kwa lengo la kuhakikisha shughuli za bandari zinakuwa salama, za ufanisi na za kuaminika.

Uwekezaji wetu endelevu katika Bandari ya Dar es Salaam unaonyesha dhamira ya muda mrefu ya DP World katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa Afrika na kuiunganisha na mifumo ya biashara ya kimataifa. Kupitia ushirikiano wetu na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), hatuboreshi tu miundombinu hii muhimu, bali pia tunawezesha mtangamano wa kikanda, kupunguza vikwazo vya kibiashara, na kutengeneza fursa endelevu za kiuchumi," anasema Mohammed Akoojee, Ofisa Mtendaji Mkuu na Mkurugenzi Mkuu wa DP World kanda ya Afrika.
Kwa taarifa zaidi kuhusu jinsi DP World inavyoboresha biashara ya kimataifa, tembelea tovuti yetu: www.dpworld.com

Kwa maswali ya vyombo vya habari, tafadhali wasiliana na;

Keitumetse Masike
Mkurugenzi: Mawasiliano ya Biashara na Mikakati Afrika
Keitumetse.masike@dpworld.com
+27 61 831 8490

Kholiswa Hashe
Meneja Mwandamizi, Mawasiliano – Afrika Mashariki
Kholiswa.Hashe@dpworld.com
+27 72 741 0099

Fuatilia DP World kupitia:



Kuhusu DP World

DP World inabadilisha mustakabali wa biashara ya kimataifa ili kuboresha maisha ya watu kila mahali. Tukifanya kazi katika mabara sita tukiwa na timu ya wafanyakazi zaidi ya 125,000, tunajumuisha miundombinu ya kimataifa na uzoefu wa maeneo husika ili kutoa huduma jumuishi za ugavi. Kuanzia Bandari na Vituo vya Huduma (Terminals) hadi Huduma za Majini, Lojistiki na Teknolojia, tunatumia ubunifu kutengeneza njia bora zaidi za kufanya biashara—huku tukipunguza changamoto kuanzia kiwandani hadi mlangoni mwa mteja.

Katika kanda ya kusini mwa jangwa la Sahara, DP World imeajiri zaidi ya watu 28,000, ina magari zaidi ya 6,300, na inafanya kazi katika masoko 48.
TUNAFANIKISHA MTIRIRIKO WA BIASHARA
Share:

BENKI YA ABSA TANZANIA YATOA SHILINGI MILIONI 20 KUSAIDIA MATIBABU YA WATOTO WENYE MAGONJWA YA MOYO

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto), akizungumza katika hafla ya utiaji saini Hati za Makubaliano (MoU) ya ushirikiano kati ya benki hiyo na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), ambapo pia benki hiyo ilitoa Shilingi Milioni 20 kusaidia matibabu ya watoto wenye changamoto ya magonjwa ya moyo wanaotoka katika familia zenye uhitaji. Hafla hiyo ilifanyika katika taasisi hiyo, jijini Dar es Salaam jana. Kutoka kushoto ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge, Meneja Mkuu wa Taasisi ya Global Medicare, Bw. Daniel Lazaro, na Ofisa Huduma za Sheria wa JKCI, Bi. Ummukulthum Said.

KATIKA kuendeleza juhudi zake za kuchangia ustawi wa jamii kupitia programu zake za uwajibikaji kwa jamii, Benki ya Absa Tanzania imetoa msaada wa Shilingi milioni 20 kwa ajili ya kusaidia matibabu ya watoto wanaoishi na magonjwa ya moyo nchini Tanzania.

Msaada huo umetolewa kupitia Heart Team Africa Foundation (HTAF), taasisi isiyo ya kiserikali iliyoanzishwa na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), yenye lengo la kuwasaidia watoto wanaotoka katika mazingira yenye uhitaji Ili kupata matibabu na huduma za moyo hivyo kuokoa maisha yao.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini wa Hati ya Makubaliano (MoU), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Obedi Laiser, alisema ushirikiano huo unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuwa chachu ya maendeleo mema katika jamii inazozihudumia.

"Dhamira yetu ni kuwa chachu ya maendeleo mema katika kila tunachofanya, na ushirikiano huu ni uthibitisho wa dhamira hiyo kwa vitendo. Tunatambua kazi kubwa inayofanywa na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete katika kutoa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo kwa watoto na familia nchini Tanzania. Kupitia Hati hii ya Makubaliano, tunaongeza fursa kwa watoto wanaoishi na magonjwa ya moyo kupata matibabu yanayookoa maisha na kuzipa matumaini familia zinazokabiliwa na changamoto kubwa za kiafya na kifedha."

"Kila mtoto anastahili nafasi ya kuishi maisha yenye afya na yenye tija. Kwa kuwekeza katika afya zao leo, tunawekeza katika mustakabali wao, ustawi wa familia zao na maendeleo endelevu ya jamii zetu. Tunajivunia kushirikiana na JKCI katika mpango huu muhimu unaolenga kuboresha maisha ya watoto kote nchini Tanzania”, alisema Bw. Laiser.

Akipokea msaada huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge, aliishukuru Benki ya Absa Tanzania kwa mchango huo, akieleza kuwa utasaidia kuongeza upatikanaji wa matibabu muhimu ya moyo kwa watoto wanaoishi na magonjwa ya moyo.

Alisema magonjwa ya moyo yanaongezeka kwa kasi duniani ikiwa ni pamoja na Tanzania, waathirika pia wakiwa ni watoto ambao wengi wao zaidi ya asilimia 70 wanazaliwa wakiwa na changamoto za magonjwa hayo licha ya wale wanaoyapata baada ya kuzaliwa.

"Msaada huu umekuja wakati muhimu kwa watoto wengi na familia zinazohitaji huduma maalumu za matibabu ya moyo," alisema. "Mbali na kutusaidia kuokoa maisha, unadhihirisha nafasi muhimu ya ushirikiano kati ya sekta binafsi na taasisi za afya katika kuimarisha utoaji wa huduma za afya na kuboresha matokeo ya matibabu kwa wagonjwa nchini Tanzania."

Namshukuru Mheshimiwa rais na serikali yake kwa kusaidia zaidi ya asilimia 70 ya gharama, kwa niaba ya bodi ya JKCI, kwa niaba ya serikali kwa jinsi mnavyofanya kumuunga mkono mheshimiwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kurudisha matumaini na kuwapa watu upendo, Absa mmefanya,mmetekeleza kile ambacho rais anakihitaji”, aliongeza Dk. Kisenge.

Nao baadhi ya wazazi wanufaika wa msaada huo, Mariam Athumani ambaye mtoto wake Lightness ameshafanyiwa upasuaji wa moyo na Adam Nuhu ambaye mtoto wake Ajmalbey anayesubiri upasuaji wametoa shukurani kwa Benki ya Absa huku wakiziomba taasisi nyingine kujitolea kuwasaidia kutokana na changamoto kubwa wanazozipata wazazi wenye watoto wenye magonjwa ya moyo.

Benki ya Absa inasema mchango huo unathibitisha dhamira ya benki hiyo ya ‘kuiwezesha Afrika ya kesho, pamoja... Hatua moja baada ya nyingine’, kupitia kusaidia upatikanaji wa matibabu yanayookoa maisha kwa watoto wenye magonjwa ya moyo, ikilenga kuboresha matokeo ya afya, kupunguza mzigo wa kifedha kwa familia zilizoathirika, na kuchangia kujenga jamii zenye afya bora na ustahimilivu zaidi nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge wakisaini Hati za Makubaliano (MoU) ya ushirikiano kati ya pande hizo mbili, katika hafla ambayo pia benki hiyo ilitoa Shilingi Milioni 20 kusaidia matibabu ya watoto wenye changamoto ya magonjwa ya moyo wanaotoka katika familia zenye uhitaji. Hafla hiyo ilifanyika katika taasisi hiyo, jijini Dar es Salaam jana. Kutoka kushoto ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi na Meneja Mkuu wa Taasisi ya Global Medicare, Bw. Daniel Lazaro.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge wakibadilishana Hati za Makubaliano (MoU) ya ushirikiano kati ya pande hizo mbili muda mfupi baada ya kuzisaini katika hafla ambayo pia benki hiyo ilitoa Shilingi Milioni 20 kusaidia matibabu ya watoto wenye changamoto ya magonjwa ya moyo wanaotoka katika familia zenye uhitaji. Hafla hiyo ilifanyika katika taasisi hiyo, jijini Dar es Salaam jana. Kutoka kushoto ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi na Meneja Mkuu wa Taasisi ya Global Medicare, Bw. Daniel Lazaro.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge (wa nne kulia) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kulia kwake), wakipiga picha ya pamoja pamoja na wazazi na watoto wao wanaopatiwa matibabu ya moyo katika taasisi hiyo mara baada ya tukio hilo jijini Dar es Salaam jana.
Share:

BENKI YA ABSA YAENDELEA KUJIZATITI KATIKA KUWAWEZESHA WAJASIRIAMALI NCHINI

Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Victor Nchimbi akizungumza na baadhi ya wajasiriamali kuhusu huduma zinazotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, katika hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.

KATIKA kutambua mchango wa wanawake wajasiriamali katika kuinua Uchumi wa Taifa, Benki ya Absa Tanzania imeendelea kuhamasisha wajasiriamali hao kujiunga na akaunti ya SHE ya benki hiyo ambayo pamoja na faida nyingine, akaunti hiyo haina makato ya mwezi ya kuendesha akaunti, ada za kufanyia miamala na kuweza kufanya miamala kwa kutumia fedha za kitanzania na za kigeni.

Akizungumza wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani, jijini Dar es Salaam hivi karibuni, ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini, Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa benki hiyo, Bw. Victor Nchimbi alisema kwa kupitia akaunti ya SHE, wanajasiriamali wanawake wanapata mafunzo maalumu ya jinsi ya kuendesha biashara zao kwa mafanikio.

Tukiwa kama wadau wakubwa wa sekta hii ya ujasiriamali na kwa kutambua mchango wa wajasiamali Tanzania tumekuwa na huduma mbalimbali tunazowapatia wajasiriamli wetu, ikiwa ni pamoja na mikopo yenye gharama nafuu, huduma za kidigitali, ukiangalia katika maadhimisho haya, waadhimishaji wengi ni wanawake, tunayo akaunti ya SHE, iliyojikita katika kuwawezesha wanawake kuichumi”, alisema.

Akizungumza katika hafla hiyo, mmoja wa wajasiriamali anayejishughulisha na biashara ya vipodozi, Bi. Maua Jumanne alisema, suala la elimu ya mitaji, mikopo na jinsi ya kufanya biashara kwa ufanisi limekuwa ni changamoto kwa wanawake wajasiriamali wengi, hivyo akatoa ushauri kwa benki mbalimbali kuyapa uzito mambo hayo.

Natoa ushauri kwa watu wa mabenki kutufikia na kutupa elimu ya mitaji na mikopo ya kutusaidia sisi wajasiriamali wadogo tuweze kukua katika biashara zetu, na kuepukana na mikopo inayotolewa na vikundi vya watoa mikopo vya kausha damu”, alisema Bi. Maua.

Benki ya Absa imeendelea kujitolea katika kuunda majukwaa yanayofikika kwa urahisi ambapo Biashara Ndogo, Ndogo za Kati na za Kati, zinaweza kubadilishana mbinu bora za biashara, kupata fursa za ufadhili, na kuhamasisha ubunifu, huku ikidumisha lengo kuu la benki hiyo la 'Kuiwezesha Afrika ya kesho, pamoja, hatua moja baada ya jingine'.
Meneja Bidhaa wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa (kulia) akizungumza kuhusu huduma zizotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, kwa baadhi ya wahudhuriaji waliofika katika banda lao, katika Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.
Ofisa Huduma kwa Wateja wa Benki ya Absa, Bi. Mboni Sabura (katikati) akizungumza na baadhi ya wajasiriamali kuhusu huduma zinazotolewa na benki hiyo hususani akaunti maalumu ya wanawake ya She, katika hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini, jijini Dar es Salaam hivi karibuni.Kulia ni Meneja Bidhaa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.
Meneja Bidhaa wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa (kulia) akizungumza kuhusu huduma zizotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, kwa baadhi ya wajasiriamali waliofika katika Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani, ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kuwezesha tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.
Baadhi ya wawezeshaji na wajasiriamali waliojitoleza kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani wakipiga picha ya pamoja mara baada ya kukamilika kwa tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Benki ya Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini hafla hiyo. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.
Share:

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

Popular Posts

Blog Archive

Labels

Blog Archive

Recent Posts

Label Cloud

BIASHARA (329) BURUDANI (4) KIMATAIFA (10) KITAIFA (129) MICHEZO (41) SIASA (3)

Pages