OWM YASISITIZA UJUMUISHWAJI WA WATU WENYE ULEMAVU KATIKA MIPANGO YA TAIFA

Na Mwandishi Wetu – Dar es Salaam | SERIKALI imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha Watu Wenye Ulemavu wanapata nafasi sawa katika nyanja zote za maendeleo, ikiwa ni pamoja na kijamii, kiuchumi na kisiasa, kupitia sera, sheria na mipango jumuishi inayotekelezwa nchini.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt. Jim Yonazi wakati wa ufunguzi wa kikao kazi kilichowakutanisha viongozi wa vyama vya Watu Wenye Ulemavu na mashirika yasiyo ya kiserikali kujadili utekelezaji wa sera, sheria na miongozo ya ujumuishaji nchini.
Amesema hatua kubwa zimeendelea kuchukuliwa katika kuhakikisha hakuna mwananchi anayeachwa nyuma, ambapo Sera ya Taifa ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2004 pamoja na Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 zimekuwa msingi muhimu wa utekelezaji wa haki na usawa kwa kundi hilo.

Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa kila sera, mpango na huduma inayotekelezwa nchini inazingatia ujumuishaji wa Watu Wenye Ulemavu tangu hatua ya upangaji, utekelezaji, ufuatiliaji hadi tathmini, ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma,” amesema Dkt. Jim Yonazi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa mawasiliano bora na uratibu imara kati ya Serikali, vyama vya Watu Wenye Ulemavu na mashirika yasiyo ya kiserikali, akibainisha kuwa ushirikiano huo ni msingi muhimu wa kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa shughuli za maendeleo.
Amesema ujumuishaji si jukumu la sekta moja pekee, bali ni wajibu wa kila taasisi, kila sekta na kila mdau wa maendeleo. “Tunapaswa kufanya kazi kwa pamoja ili kuhakikisha huduma zote zinamfikia kila mwananchi kwa usawa,” alisisitiza.

Dkt. Yonazi pia ametoa wito wa kuimarishwa kwa mifumo ya mawasiliano inayowezesha Watu Wenye Ulemavu kupata taarifa kwa urahisi, ikiwemo matumizi ya lugha ya alama, maandishi ya Breli, teknolojia saidizi na mifumo mingine jumuishi.

Serikali inatambua mchango mkubwa unaotolewa na vyama vya Watu Wenye Ulemavu pamoja na mashirika yasiyo ya kiserikali katika kutoa huduma za utetezi wa haki, elimu kwa umma, mafunzo ya kujenga uwezo, uwezeshaji kiuchumi, huduma za afya, elimu jumuishi na ushauri wa kitaalamu,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Yonazi amesema kuwa pamoja na jitihada ambazo Serikali imeendelea kuzichukua, bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazohitaji ushirikiano wa wadau wote.
Amesema changamoto hizo ni pamoja na uelewa usioridhisha kuhusu masuala ya ujumuishaji katika baadhi ya sekta, utekelezaji usiofanana wa sera na sheria, pamoja na changamoto za upatikanaji wa huduma jumuishi zinazokidhi mahitaji ya Watu Wenye Ulemavu.

Kutokana na hali hiyo, kikao hiki ni muhimu sana kwa kuwa kinatoa fursa ya kujadili kwa kina namna bora ya kuimarisha ujumuishaji wa huduma katika sekta zote.

Awali, Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA), Bi. Tungi Mwanjala, ameiomba Serikali kuendelea kuangalia uwezekano wa kuwatambua watoto wa wazazi wenye ulemavu ili waweze kunufaika na fursa mbalimbali za maendeleo, ikiwemo kupata mikopo ya elimu ya juu kwa urahisi.
Bi.Mwanjala ameeleza kuwa, Serikali imepiga hatua kubwa kwa kukamilisha muongozo na mfumo wa utambuzi wa watu wenye ulemavu, lakini bado kuna haja ya kupanua utambuzi huo kwa watoto wa wazazi wenye ulemavu.

"Tunashukuru Serikali kwa kukamilisha muongozo na mfumo wa kutambua watu wenye ulemavu. Hata hivyo, tunaomba pia watoto wetu watambuliwe kupitia mfumo maalumu utakaowezesha kupata vitambulisho, jambo litakalowarahisishia kupata mikopo ya elimu ya juu na fursa nyingine za maendeleo ikiwamo ajira kwa kuzingatia utaratibu uliopo," amesema.
Share:

RAIS DKT. MWINYI: TAASISI ZA KIFEDHA ZA NDANI ZINAFAA KUIMARISHA USHIRIKIANO NA SERIKALI KATIKA MIRADI YA MAENDELEO

  

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akimkabidhi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia), tuzo ya kumbukumbu kama ishara ya kuthamini ushirikiano imara kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta ya fesha pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi visiwani humo. Ilikuwa wakati wa ziara ya Mkurugenzi huyo pamoja na ujumbe wake, Ikulu, mjini Zanzibar, juzi.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesisitiza kuwa bado kuna fursa nyingi kwa taasisi za kifedha za ndani kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Rais Dkt. Mwinyi alitoa kauli hiyo jana alipokutana na ujumbe wa Absa Bank Tanzania, ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw. Obeid Laiser, aliyefanya ziara ya heshima Ikulu Zanzibar.

Amesema Serikali iko tayari kushirikiana kwa karibu na benki za ndani zinazodhihirisha dhamira ya kusaidia jitihada za maendeleo, hususan katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya kiuchumi na kijamii katika sekta mbalimbali.

Rais Dkt. Mwinyi aliipongeza Absa Bank Tanzania kwa utayari wake wa kushirikiana na Serikali na kuchangia maendeleo ya Zanzibar. Aidha, alieleza kuwa Serikali imeimarisha mifumo ya kufadhili miradi ya maendeleo kwa kupanua vyanzo vya fedha nje ya bajeti ya kawaida, hatua inayolenga kuharakisha utekelezaji wa miradi na kuongeza ufanisi.

Rais aliwahakikishia viongozi wa benki hiyo kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za kifedha katika kurahisisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo kupitia mikopo na mipango mingine ya kifedha.

Kwa upande wake, Bw. Obeid Laiser alishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ushirikiano wake wa kudumu na benki hiyo na kumpongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa uongozi wake uliosababisha maendeleo makubwa Zanzibar. Alisisitiza tena dhamira ya Absa Bank Tanzania kuendeleza ushirikiano na Serikali katika kusaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi na uchumi wa Zanzibar.

Bw. Laiser pia alieleza mchango wa Absa katika uchumi wa Zanzibar, akibainisha ueneaji na athari zake kupitia utoaji wa huduma za kifedha kwa watu binafsi, wafanyabiashara na mashirika makubwa.

Katika taarifa iliyotolewa baada ya mkutano huo, Bw. Laiser alieleza shukrani za benki kwa Serikali ya Zanzibar kwa kuunda mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji.

Tunajivunia kupata fursa ya kukutana na Mheshimiwa Rais Hussein Ali Mwinyi na kujadili safari ya maendeleo ya kipekee ya Zanzibar. Kama mshirika wa kifedha anayeaminika, Absa itaendelea kujitolea kusaidia matarajio ya wananchi wa Zanzibar kupitia upatikanaji wa fedha, urahisishaji wa uwekezaji, ukuzaji wa ujasiriamali na suluhisho bunifu za kibenki zinazochangia katika ukuaji endelevu wa uchumi.

Absa inahudumia zaidi ya wateja 11,000 Zanzibar, inasimamia amana zinazozidi TZS bilioni 136 na imekopesha zaidi ya TZS bilioni 64 kwa watu binafsi, biashara ndogo na za kati pamoja na makampuni makubwa yanayofanya kazi katika sekta kuu za uchumi ikiwemo utalii, hoteli, biashara na uchuuzi,” alisema Bw. Laiser.

Bw. Laiser pia alisisitiza mchango wa Absa nje ya huduma za kibenki kupitia miradi ya uwajibikaji wa kijamii, ikiwemo kusaidia afya ya mama na mtoto chini ya mpango wa Uzazi ni Maisha, unaotekelezwa kwa ushirikiano na AMREF Health Africa na Wizara ya Afya Zanzibar. Kupitia mpango huu, Absa imechangia kuboresha upatikanaji wa vifaa muhimu vya kitabibu na kuimarisha huduma salama za kujifungua kwa akina mama na watoto wachanga Zanzibar.

Absa Bank Tanzania itaendelea kujitolea kwa dhima yake ya 'Kuiwezesha Afrika ya kesho pamoja… hatua moja baada ya nyingine' na kusaidia ustawi wa muda mrefu na mafanikio ya wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akizungumza na ujumbe kutoka Benki ya Absa Tanzania, ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw, Obedi Laiser (wa tano kushoto), ulipomtembelea Ikulu, Zanzibar juzi. Bw. Laiser alitoa shukurani za benki kutokana na ushirkiano uliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta za kibenki nchini pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi yanayofanyika visiwani humo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (Katikati), akipiga picha ya kumbukumbu na ujumbe kutoka Benki ya Absa Tanzania, ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw, Obedi Laiser (kulia kwake), ulipomtembelea Ikulu, Zanzibar juzi. Wakati wa mazungumzo yao, Bw. Laiser alitoa shukurani za benki kutokana na ushirkiano uliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta za kibenki nchini pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi yanayofanyika visiwani humo. (PICHA NA IKULU)
Share:

DCB YAZINDUA KAMPENI YA "TUMA BURE, SHINDA KILA WIKI" KUVUTIA WATEJA WA HUDUMA ZA KIDIJITALI

 

DAR ES SALAAM: Benki ya DCB imezindua kampeni maalum ya miezi sita ijulikanayo kama "Tuma Bure, Shinda Kila Wiki", inayolenga kuhamasisha matumizi ya huduma za kidijitali na kuongeza ujumuishaji wa huduma za kifedha nchini kwa kuwapatia wateja nafasi ya kushinda zawadi mbalimbali huku wakifanya miamala bila kutozwa gharama.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya DCB, Sabasaba Moshingi, amesema benki hiyo imefanya maboresho makubwa ya huduma zake za kidijitali baada ya kubaini kuwa wateja wengi wanahitaji huduma za haraka, salama, nafuu na zinazopatikana muda wote. Amesema kupitia mfumo mpya wa DCB Pesa App, wateja wanaweza kufungua akaunti popote walipo nchini na kufanya miamala mbalimbali bila makato.
Moshingi amesema kampeni hiyo pia inalenga kuunga mkono juhudi za Serikali za kuongeza ushiriki wa wananchi katika huduma rasmi za kifedha, huku akiwahimiza Watanzania kutumia huduma za benki ili kukuza biashara zao na kufikia malengo ya kiuchumi kwa urahisi zaidi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko wa DCB, Geofrey Magugi, amesema mteja anayefungua akaunti kupitia DCB Pesa App na kufanya angalau muamala mmoja ataingia kwenye droo ya kila wiki yenye zawadi ya Shilingi 100,000 kwa washindi 10,amesema wateja watakaofanya miamala zaidi ya mitatu kwa mwezi watapata nafasi ya kushinda zawadi kubwa zaidi ikiwemo Shilingi milioni moja kila mwezi.

Naye Mkurugenzi wa Biashara wa DCB, Ramadhani Mganga, amesema kampeni hiyo itadumu hadi Desemba mwaka huu na inalenga kuwazawadia wateja wanaotumia huduma za benki kwa njia za kidijitali, amesema DCB imeendelea kuwa miongoni mwa taasisi za fedha zinazoweka kipaumbele katika ubunifu wa huduma nafuu, huku ikitoa fursa kwa Watanzania kufungua akaunti na kufanya miamala kutoka mahali popote nchini bila kulazimika kutembelea matawi ya benki.
Mganga amesema pamoja na faida ya kutuma fedha bila makato, wateja watakaoshiriki kampeni hiyo watakuwa na nafasi ya kushinda zawadi za kila wiki, kila mwezi na zawadi kubwa itakayotolewa mwishoni mwa kampeni mwezi Desemba, akiwataka Watanzania kuchangamkia fursa hiyo kwa kufungua akaunti za DCB na kutumia huduma zake za kidijitali.
Share:

BENKI YA ABSA YAUNGANA NA TPSF KUWANOA WAJASIRIAMALI WANAWAKE

Meneja Miradi wa Benki ya Absa, Bi. Munira Chambuso akizungumza katika semina iliyoandaliwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, ikihuhusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.

DAR ES SALAAM | Wanawake wafanyabiashara kutoka sekta mbalimbali nchini wamehimizwa kuendelea kujengewa uwezo wa elimu ya fedha ili kuwawezesha kufanya maamuzi sahihi ya kifedha, kukuza biashara zao na kuongeza mchango wao katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa na Meneja wa Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi, wakati wa mafunzo ya elimu ya fedha yaliyoandaliwa kwa ushirikiano kati ya Benki ya Absa Tanzania na Shirikisho la Sekta Binafsi Tanzania (TPSF).

Akizungumza katika mafunzo hayo, Bi. Lukuvi amesema mpango huo ulianza mwaka jana kama sehemu ya ajenda ya uwajibikaji kwa jamii ya benki hiyo, inayolenga kuwawezesha wananchi, hususan wanawake wajasiriamali, kupata maarifa ya kifedha yatakayowasaidia kuwekeza kwa ufanisi na kuimarisha biashara zao.

Amesema mafunzo hayo yamewakutanisha wanawake wamiliki wa biashara kutoka sekta mbalimbali kwa lengo la kuwapa elimu kuhusu usimamizi wa fedha, uwekezaji na mikakati ya kuongeza mapato pamoja na kukuza biashara zao kwa njia endelevu.

Tunafurahi kuona wanawake wengi wakishiriki mafunzo haya. Tunaamini elimu ya fedha ni nyenzo muhimu katika kuwajengea uwezo wa kufikia mafanikio ya kiuchumi na kuimarisha ustawi wa biashara zao,” amesema Bi. Lukuvi.

Aidha, ameishukuru TPSF kwa ushirikiano wake katika kufanikisha mafunzo hayo na kubainisha kuwa ushirikiano huo utaendelea ili kuwafikia wanawake wengi zaidi na kuwapa fursa ya kupata elimu ya fedha na uwekezaji.

Mafunzo hayo yamewaleta pamoja wanawake kutoka sekta mbalimbali ikiwemo biashara, viwanda vidogo, madini, utalii, sekta za ubunifu na ukandarasi, wakiwakilisha wanachama wa TPSF.

Katika mafunzo hayo, wataalamu wa Absa walitoa elimu kuhusu usimamizi wa fedha ikijumuisha masuala ya bajeti, akiba na uwekezaji kwa lengo la kusaidia wajasiriamali kukuza biashara zao na kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kiuchumi.

Kwa upande wake, mwakilishi wa TPSF, Kinanasi Seif, amesema shirikisho hilo litaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuwawezesha wanawake wajasiriamali kupitia programu za mafunzo na elimu zinazolenga kukuza biashara na kuimarisha uchumi wao.

Amesema TPSF imekuwa ikitekeleza programu mbalimbali za kuwawezesha wanawake katika nyanja tofauti za biashara huku ikitambua mchango mkubwa wa wanawake katika maendeleo ya sekta binafsi na uchumi wa taifa kwa ujumla.

Tumefanikiwa kuwaleta pamoja wanawake wajasiriamali kutoka vyama mbalimbali ili wapate mafunzo ya elimu ya fedha na uwekezaji kutoka Benki ya Absa. Tunaamini maarifa haya yatawasaidia kufanya maamuzi sahihi ya kifedha na kukuza biashara zao,” amesema Seif.

Ameongeza kuwa ushirikiano kati ya TPSF na Benki ya Absa ni hatua muhimu katika kuhakikisha wanawake wanapata fursa za kujengewa uwezo na kufikia maendeleo endelevu katika shughuli zao za kiuchumi.

Wakati huo huo, wataalamu kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) walitoa elimu kuhusu utii wa kodi kwa biashara ndogo na za kati (SMEs), wakisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria za kodi katika kujenga biashara imara na endelevu.

Akizungumza katika semina hiyo, Afisa wa TRA, Zephaniah Usange Jamange, amesema kuwa pamoja na walipakodi kutekeleza wajibu wao wa kulipa kodi, ni muhimu pia kufahamu haki zao wanazostahili kupata kutoka kwa mamlaka hiyo.

Amesema miongoni mwa haki hizo ni usiri wa taarifa za kikodi, ambapo taarifa zote zinazowasilishwa na mlipakodi zinapaswa kubaki siri na haziwezi kutolewa kwa watu wasiohusika. Aidha, walipakodi wote wanapaswa kuhudumiwa kwa usawa bila upendeleo wowote.

Walipakodi pia wana haki ya kupinga maamuzi yanayotolewa na maafisa wa kodi pale wanapoona hawajaridhika nayo. Maamuzi ya awali si ya mwisho, hivyo kuna fursa ya kukata rufaa kwa kufuata taratibu zilizowekwa,” amesema Jamange.

Kwa upande wa wajibu, TRA imewakumbusha wafanyabiashara kuhakikisha wanajisajili kwa TIN ndani ya siku tano tangu waanze biashara. Pia wafanyabiashara wanaofikia mauzo yanayostahili kwa mujibu wa sheria wanapaswa kutumia mashine za kutolea risiti za kielektroniki (EFD) na kujisajili kwa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) pale inapohitajika.

Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za pamoja za kukuza ushiriki wa wanawake katika shughuli za kiuchumi kwa kuwapatia ujuzi wa usimamizi wa fedha, uwekezaji, utii wa kodi na uendeshaji bora wa biashara, hatua inayotarajiwa kuchochea ukuaji wa biashara zao na maendeleo ya uchumi wa taifa.
Meneja wa Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (wa pili kutoka kushoto), akizungumza na baadhi ya washiriki, katika semina iliyoandaliwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati ikihusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.
Mkurugenzi wa Wanachama wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Bi. Kinanasy Seif akizngumza katika semina iliyoandaliwa na Benki ya Absa Tanzania kwa kushirikiana na taasisi hiyo kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, ikihusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.
Meneja Bidhaa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa, akizungumza katika semina iliyoandaliwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, Ikihusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.
Ofisa Elimu kwa Mlipa Kodi na Mawasiliano wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Zephania Mange, akitoa elimu kuhusu wajibu wa mlipa kodi katika semina iliyoandaliwa na Benki ya Absa Tanzania kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), kwa wanawake wajasiriamali wadogo na wa kati, Ikihusu elimu ya fedha na usimamizi wa uwekezaji, jijini Dar es Salaam jana.
Wawakilishi kutoka Benki ya Absa na TPSF, wakipiga picha ya kumbukumbu pamoja na washiriki wa semina hiyo pamoja na wawezeshaji wengine, mara baada ya kumalizika kwa semina hiyo, jijini Dar es Salaam jana.
Share:

ABSA BANK TANZANIA YAWAPA WAWEKEZAJI WA TAASISI MAARIFA YA UCHUMI NA MASOKO

Mkurugenzi wa Kitengo cha Masoko ya Fedha za Kigeni wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Irene Rwegalulira (kulia), na Mtaalamu Mwandamizi wa Masuala ya Biashara kutoka Absa Group, Bw. Gerald Nana (kushoto) wakizungumza na baadhi ya washiriki kutoka taasisi kubwa za uwekezaji wakati ya warsha ya siku moja iliyoandaliwa na benki hiyo ili kutoa mwelekeo wa kiuchumi wa ndani na nchi nyingine mbalimbali duniani, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.

Benki ya Absa Tanzania jana imeandaa semina ya ngazi ya juu kwa wawekezaji wa taasisi, ikiwakutanisha wadau muhimu kutoka kampuni za bima, taasisi za fedha ndogo, wasimamizi wa mifuko ya uwekezaji, madalali wa masoko ya fedha na mifuko ya hifadhi ya jamii kujadili mwelekeo wa uchumi wa Tanzania pamoja na mwenendo unaojitokeza katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Warsha hiyo, iliyowavutia wawakilishi kutoka taasisi zisizo za kibenki za huduma za kifedha, wadhibiti wa sekta na viongozi wa tasnia mbalimbali, ililenga kuwapatia wawekezaji maarifa ya vitendo kuhusu namna ya kukabiliana na mazingira ya uchumi wa dunia yanayozidi kuwa magumu kutokana na mabadiliko ya viwango vya riba, kuyumba kwa thamani za sarafu pamoja na hali ya kutokuwa na uhakika wa kisiasa na kiuchumi duniani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, Mkurugenzi wa Masoko ya Fedha za Kigeni wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Irene Rwegalulira, alisisitiza umuhimu wa maandalizi na kufanya maamuzi ya kimkakati katika mazingira ya masoko yanayobadilika kwa kasi.

Mafanikio katika mazingira ya sasa hayategemei uwezo wa kutabiri kila mabadiliko ya soko. Kinachohitajika ni kuwa tayari, kulindwa na kuwa katika nafasi nzuri wakati mabadiliko yanapotokea,” alisema.

Bi. Irene alisema kuwa licha ya mabadiliko yanayoendelea katika uchumi wa dunia na wa ndani ya nchi, bado kuna fursa kwa wawekezaji watakaokuwa na taarifa sahihi pamoja na mikakati madhubuti ya usimamizi wa hatari.

Alisisitiza tena dhamira ya Absa ya kuendelea kuwasaidia wateja wake wa taasisi kupitia utaalamu wa masoko, suluhisho bunifu za kifedha na ushauri wa kimkakati.

Jukumu letu kama mshirika wenu katika Masoko ya Kimataifa ni kuwasaidia kukabiliana na hali ya kutokuwa na uhakika, kusimamia hatari kwa ufanisi na kutumia fursa zilizopo kwa kujiamini na kwa usahihi,” alisema.

Warsha hiyo iliandaliwa kwa ushirikiano na Shirika la Tanzania Reinsurance Corporation (Tan Re), ambapo mchango wake katika kuimarisha sekta ya bima na huduma za kifedha nchini kupitia usimamizi madhubuti wa hatari ulitambuliwa wakati wa hafla hiyo.

Mtaalamu huyo wa Masoko ya Fedha Kimataifa kutoka Absa pia alizipongeza taasisi za udhibiti, zikiwemo Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) na Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kwa mchango wao endelevu katika kujenga imani ya washiriki wa soko na kuunga mkono ukuaji endelevu wa sekta ya fedha.

Tukio hilo pia lilinufaika na ushiriki wa wataalamu wa Absa kutoka masoko mbalimbali barani Afrika, waliohudhuria ana kwa ana na kwa njia ya mtandao, jambo lililoonyesha kuongezeka kwa muunganiko wa masoko ya fedha barani humo pamoja na umuhimu wa kubadilishana maarifa.

Wakati wa semina hiyo, washiriki walipatiwa mawasilisho kuhusu mwenendo wa uchumi mpana unaoathiri Tanzania na dunia kwa ujumla, mikakati ya kusimamia hatari zinazotokana na mabadiliko ya viwango vya ubadilishaji fedha za kigeni na viwango vya riba, pamoja na suluhisho za uwekezaji zinazolenga kuongeza faida ya uwekezaji huku zikizingatia viwango vya hatari vinavyokubalika kwa taasisi husika.

Kwa mujibu wa Absa, kikao hicho ni sehemu ya dhamira pana ya benki hiyo ya kuwawezesha wawekezaji kupitia taarifa na uchambuzi wa masoko unaoweza kutumika moja kwa moja katika kufanya maamuzi, pamoja na kuimarisha ushirikiano wa muda mrefu na wateja wake wa taasisi.

Kikiwa kimeandaliwa chini ya Lengo la Benki ya Absa la “Kuiwezesha Afrika ya Kesho, pamoja... Hatua moja baada ya nyingine,” semina hiyo ililenga kuwapatia wawekezaji maarifa na nyenzo zinazohitajika kufanya maamuzi sahihi katika mazingira ya soko yanayobadilika na kutumia fursa mpya zinazojitokeza ndani na nje ya Tanzania.

Mmoja wa washiriki katika semina hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Ushauri wa Kifedha ya Exodus Advisory, Bw. Ramadhan Kagwandi alishauri kutokana na Athari za kiuchumi zinazotokana na majanga ya kidunia hususani suala la kupanda kwa bei ya mafuta akisema juhudi hazina budi kufanyika katika kufanya uwekezaji mkubwa katika matumizi ya nishati mbadala wa mafuta, hususani matumizi ya gesi.

La pili serikali inapaswa kuangalia namna nchi yetu inaweza kuwa na akiba ya kutosha ya mafuta endapo tutahitai kuendelea kutumia nishati hiyo, lakini lingine likiwa ni suluhisho la muda mrefu kama nchi ni kuwa na Uchumi unaojitegemea, na hili naona serikali imeshalifanyia kazi katika Bajeti ya 2026/2026 ikionesha kuwa asilimia karibu 75 ya bajeti inategemea vyanzo vya ndani,” alisemwa Bw. Kagwandi.

Kwa upande wake mshiriki mwingine, Bw. Beatus Mlingi, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Diamond Global Securities alitoa shukurani kwa Benki ya Absa kwa kuwa na ubunifu katika kuandaa semina hiyo, kwani imewasaidia kupata masuluhisho mengine ya jinsi ya kuweza kufanya biashara zao kwa ufanisi licha changamoto mbalimbali zinazojitokeza.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Masoko ya Fedha za Kigeni wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Irene Rwegalulira akizungumza na baadhi ya washiriki kutoka taasisi kubwa za uwekezaji, wakati akifungua rasmi warsha ya siku moja iliyoandaliwa na benki hiyo ili kutoa mwelekeo wa kiuchumi wa ndani na nchi nyingine mbalimbali duniani, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Mtaalamu Mwandamizi wa Masuala ya Biashara kutoka Absa Group, Bw. Kabelo Bogopa akizungumza na baadhi ya washiriki kutoka taasisi kubwa za uwekezaji wakati ya warsha ya siku moja iliyoandaliwa na benki hiyo ili kutoa mwelekeo wa kiuchumi wa ndani na nchi nyingine mbalimbali duniani, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Mkuu wa Masoko ya Fedha za Kigeni wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Elisia Temu (kulia) akizungumza na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Exodus Advisory, Bw. Ramadhani Kagwandi wakati ya warsha ya siku moja iliyoandaliwa na benki hiyo ili kutoa mwelekeo wa kiuchumi wa ndani na nchi nyingine mbalimbali duniani, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Masoko ya Fedha za Kigeni wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Irene Rwegalulira (katikati) akipiga picha ya pamoja na washiriki kutoka taasisi kubwa za uwekezaji na wafanyakazi kutoka benki hiyo hiyo, wakati ya warsha ya siku moja iliyoandaliwa na Benki ya Absa, ili kutoa mwelekeo wa kiuchumi wa ndani na nchi nyingine mbalimbali duniani, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Share:

BENKI YA ABSA TANZANIA YAENDELEZA HUDUMA ZA AFYA YA MAMA NA MTOTO KUPITIA UTOAJI WA VIFAA VYA HOSPITALI

  

Meneja wa Huduma za Jamii na Matuko wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (wa pili kutoka kushoto), akikabidhi vifaa vya hospitali kwa Muuguzi Kiongozi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja, Bi. Shufaa Kaniki (kulia), katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana. Kushoto ni Makamu wa Rais wa The Runners Club, Bw. Godfrey Mwangungulu, pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa hospitali. Utoaji huu wa vifaa, wenye lengo la kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto, umefuatia mafanikio ya mbio za Absa Dar City Marathon zilizofanyika tarehe 3 Mei 2026 jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wafanyakazi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja wakionesha vifaa vipya vya hospitali walivyokabidhiwa na Meneja Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (kushoto), katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana. Utoaji huu, wenye dhamira ya kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto, umewezekana kufuatia mafanikio ya mbio za Absa Dar City Marathon zilizofanyika tarehe 3 Mei 2026, jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Rais wa The Runners Club, Bw. Godfrey Mwangungulu, akitoa hotuba yake wakati wa hafla ya makabidhiano ya vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Benki ya Absa Tanzania jijini Dar es Salaam jana. Mchango huu Kutoka Benki ya Absa, wenye lengo la kuunga mkono huduma za afya ya mama na mtoto, umewezekana kufuatia mafanikio ya mbio za Absa Dar City Marathon zilizofanyika tarehe 3 Mei 2026 jijini Dar es Salaam.
Muuguzi Kiongozi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja, Bi. Shufaa Kaniki, akitoa shukrani zake baada ya kupokea msaada wa vifaa vya hospitali kutoka kwa Meneja Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (kushoto), katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana. Utoaji huu, unaolenga kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto, umefuatia mafanikio ya mbio za Absa Dar City Marathon zilizofanyika tarehe 3 Mei 2026 jijini Dar es Salaam.
Share:

BENKI YA ABSA TANZANIA NA WWF WAPANDA MITI KUADHIMISHA SIKU YA MAZINGIRA

Mkurugenzi wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Aron Luhanga (kushoto), Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja na Huduma za Kidigitali wa Benki ya Absa Tanzania, Samuel Mkuyu (katikati), na Mhifadhi Misitu wa Wilaya ya Kisarawe, Bw. Baraka Mtewa wakishirikiana kupanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, kwa kushirikiana na Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na shirika hilo.

KATIKA kuadhimisha Siku ya Mazingira Duniani, wafanyakazi wa Benki ya Absa kwa kushirikina Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), wamepanda miti 1300 katika Msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani mwishoni mwa wiki huku benki hiyo ikiahidi kuyafanya matukio hayo kuwa endelevu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Aron Luhanga alisema suala la upandaji miti ni jambo muhimu sana katika suala zima la uhifadhi wa mazingira kutokana na faida mbalimbali zinazotokana na misitu.

Benki ya Absa lengo lake kuu linasema ‘Kuiwezesha Afrika ya Kesho, Pamoja, Hatua Moja Baada ya Nyingine’, kwa kupanda miti katika eneo hili la Pugu Kazimzumbwi, tunaamini tunasaidia kuwawezesha wakazi wa Dar es Salaam kuwa na afya njema inayotokana na hewa safi kutoka mahali hapa kwani Kazimzumbwi ndio mapafu yanayolifanya jiji la Dar es salaam lipumue kwa kufyonza hewa chafu inayotoka humo."

Absa pia tunasema, Stori yako ina Thamani’ tunaamini kila stori ya mtanzania ina thamani sana kwetu, hivyo kwa kuja kupanda miti tukishirikiana na Shirika la WWF, tunaamini tumekuja kuandika Stori ya Jiji la Dar es salaam kwa kuhakikisha kwamba miti hii tunayopanda inawezesha utoaji wa hewa safi, kuleta chanzo cha mvua na kuleta mandhari nzuri na kuwa sehemu nzuri ya kutembelea,” alisema Bw. Luhanga.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Utawala wa Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), Bw. Manyerere Wajama, akimwakilisha mkurugenzi wa shirika hilo katika hafla hiyo alisema kwa kushirikia na Benki ya Absa tukio ni uwekezaji mkubwa katika suala la hewa safi na utunzaji wa mazingira, na pia msitu huo ni rasilimali kubwa kwa wakazi wa Kisarawe, kwenye hewa safi kwa sababu msitu unanyonya hewa chafu, kwenye ecology ya mazingira na pia msitu wa Pugu Kazimzumbwi ni muhimu kwenye kusaidia shughuli za wananchi wa eneo la kisarawe na maeneo Jirani.

Kwa kupanda miti tunawekeza katika maisha ya baadae ya watoto wetu, kwa sababu kwa kuhifadhi mazinigira leo tunategemea watu wataendelea kuishi kwenye mazingira safi na salama, tunahitaji ushirikiano, serikali, sekta binafsi pamoja na wakazi wa eneo hili, leo tukiondoka mwanajamii akaingiza mifugo yake maeneo haya tunakuwa hatujafanya kitu chochote, kwahiyo ili kazi yetu iwe na maana tunatakiwa tushirikiane,” alisema Bw. Wajama akitoa shukurani kubwa kwa Benki ya Absa kwa kuwa wadau wao muhimu katika suala la uhifadhi wa mazingira.

Awali Naibu Ofisa Misitu wa Wilaya ya Kisarawe, Bw. Idd Mbaruku alisema zoezi la upandaji wa miti 1300 kutoka Benki ya Absa wakishikiana na WWF ni muendelezo wa jitihada ya utunzaji wa mazingira hasa katika hifadhi yao ya Pugu Kazimzumbwi huku wakishirikiana karibu na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).

Kama inavyoelezwa msitu huu ndio mapafu ya jiji letu la Dar es Saalam, lakini pia ndio mbavu za wilaya yetu ya Kisarawe kutokana na umuhimu wake kwa sababu hapa tupo karibu sana na Dar es salaam na kama tunavyojua jiji hilo lina viwanda vingi, kuna mchafuko mkubwa wa hali ya hewa, kwahiyo msitu huu umekuwa ni sehemu ya kufyonza hiyo hewa chafu, kwa hiyo sisi kama serikali kwa kushirikiana na jamii inayotuzunguuka tutahakikisha miti hii iliyopandwa inazidi kukua,” alisema Bw. Mbaruku.
Mkurugenzi wa Masoko na Mawasiliano wa benki hiyo, Bw. Aron Luhanga (kushoto), na Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja na Huduma za Kidigitali wa Benki ya Absa Tanzania, Samuel Mkuyu, wakipanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, kwa kushirikiana na Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na Shirika la WWF.
Meneja Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (kushoto) na Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Utawala wa Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), Bw. Manyerere Wajama, wakipanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na Shirika la WWF.
Meneja Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (kulia), Mhifadhi Misitu wa Wilaya ya Kisarawe, Bw. Baraka Mtewa na Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Utawala wa Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), Bw. Manyerere Wajama, wakishirikiana kupanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na Shirika la WWF.
Baadhi ya wafanyakazi wa Benki ya Absa Tanzania walipanda miti, kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, kwa kushirikiana na Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na shirika hilo.
Wafanyakazi na viongozi wa Benki ya Absa Tanzania, wawakilishi kutoka Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), Viongozi wa Kiserikali kutoka Wilaya ya Kisarawe, wawakilishi kutoka Ofisi ya Misitu wilaya, Wakala wa Misitu (TFS), na wadau wengine wa mazingira wakipozi kwa picha ya kumbukumbu muda mfupi baada ya kukamilika kwa zoezi la upandaji miti katika Msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, Mkoani Pwani jana, kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.
Share:

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

Popular Posts

Blog Archive

Labels

Blog Archive

Recent Posts

Label Cloud

BIASHARA (327) BURUDANI (4) KIMATAIFA (10) KITAIFA (126) MICHEZO (41) SIASA (3)

Pages