DKT. YONAZI AWAKUMBUSHA VIJANA KULINDA AFYA ZAO KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UKIMWI

Na. Mwandishi Wetu - Kazuramimba Kigoma

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, Amewaasa vijana kulinda afya zao na kuepuka tabia hatarishi ili kupunguza maambukizi mapya ya VVU, kwa kuzingatia kuwa ni kundi linaloongoza kuwa hatarini zaidi nchini Tanzania.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Afua za UKIMWI Wilaya ya Uvinza Mkoa wa Kigoma alipoambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania, Dkt. Adam Mrisho, timu ya wataalam kutoka Ofisi yake, Wizara ya Afya, TAMISEMI na Ofisi ya Mkoa huo.

Aidha amepata wasaa kutembelea Kituo cha Maarifa Kata ya Kazuramimba mkoani humo kinachotoa huduma za masuala ya VVU na UKIMWI, na kukutana na vijana wanaotekeleza afua za UKIMWI kupitia vikundi vya uzalishaji mali kwa lengo la kujiinua kiuchumi na kujiletea maendeleo yao.

Akiwa katika kituo hicho, Dkt. Yonazi amepokea taarifa kutoka kwa mwenyekiti wa kikundi, Billy Sekibaha, kuhusu shughuli zinazofanywa na kikundi hicho ikiwemo za biashara ndogondogo za kuuza dagaa pamoja na shunguli za ushonaji wa nguo kwa lengo la kujikwamua kiuchumi na kuondokana na dhana ya utegemezi.

Amesisitiza kuwa, kundi la vijana linategemewa na Taifa katika shughuli za uzalishaji mali na kujiletea maendeleo yao na Taifa kwa ujumla hivyo ni vyema vijana wakaendelea kujilinda na kulinda wengine kwa kutambua hali zao na endapo wakagundulika kuwa na maambukizi ya VVU inashauriwa kuanza kutumia dawa mapema.

"Mnafanya kazi nzuri sana, endeleeni kuchangamkia uwepo wa mitandao ya kijamii kutangaza bidhaa zenu ili kuwafikia wateja wengi zaidi na kujitangaza kitaifa na kimataifa," alisisitiza Dkt. Yonazi

Kwa upande wake Mtendaji wa TACAIDS, Dkt. Adam Mrisho amewapongeza vijana hao kwa kazi nzuri wanazofanya na kusisitiza kuwa Tume itaendelea kuwawezesha vijana kiuchumi na kuwajengea uwezo ili kuendeleza mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya VVU na kufikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.
Share:

ABSA TANZANIA YAONGEZA JUHUDI ZA KUWAWEZESHA WASICHANA KATIKA TEKNOLOJIA KUPITIA GIRLCODE HACKATHON

Zandile Mkwanazi

Benki ya Absa Tanzania, kwa kushirikiana na GirlCode, shirika lisilo la kiserikali lenye makao yake nchini Afrika Kusini linalolenga kuwawezesha wasichana kutoka mazingira yenye changamoto kwa kuwapatia ujuzi na rasilimali za kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika sekta ya teknolojia, imetangaza kurejea kwa mashindano ya GirlCode Tanzania Hackathon kwa mwaka wa pili mfululizo.

Hatua hiyo inafuatia mafanikio makubwa yaliyopatikana mwaka 2025, ambapo timu ya Tanzania iliibuka na tuzo kuu ya Pan-African Grand Prize yenye thamani ya Dola za Marekani 5,000.

GirlCode Hackathon ni sehemu ya mpango mpana wa GirlCode unaolenga kuwawezesha wanawake vijana barani Afrika kwa kuwapatia ujuzi wa vitendo katika teknolojia, kuwaunganisha na walezi na wataalamu kupitia programu za ushauri, pamoja na kuwapa fursa ya kubuni suluhisho zinazolenga kukabiliana na changamoto halisi katika jamii zao.

Kurudi kwa mashindano hayo nchini Tanzania kunatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha kizazi cha wataalamu wanawake katika teknolojia na kujenga juu ya mafanikio yaliyopatikana na washiriki wa Tanzania mwaka jana.

Ushindi wa Tanzania mwaka 2025 ulidhihirisha umuhimu wa kuwekeza kwa wanawake vijana kama wabunifu, wajenzi wa suluhisho na watatuzi wa changamoto. Mafanikio hayo hayakuweka tu Tanzania katika ramani ya GirlCode Hackathon barani Afrika, bali pia yalitoa hamasa kwa wanawake vijana zaidi nchini kujiona kuwa sehemu ya uchumi wa kidijitali unaokua barani Afrika.

Akizungumzia kurejea kwa mpango huo nchini Tanzania, Ofisa Mtendaji Mkuu wa GirlCode, Zandile Mkwanazi, alisema shirika hilo linajivunia mafanikio yaliyopatikana na timu ya Tanzania mwaka jana.

GirlCode inajivunia sana kile ambacho timu ya Tanzania ilifanikiwa kukipata mwaka jana. Kushinda tuzo kuu ya Pan-African Grand Prize kumeonyesha kiwango cha vipaji, ubunifu na uwezo uliopo miongoni mwa wanawake vijana nchini Tanzania,” alisema.

Aliongeza kuwa kurejea kwa mashindano hayo kwa mwaka wa pili kunalenga kujenga juu ya mafanikio yaliyopatikana na kuwapa wanawake vijana zaidi fursa ya kuendeleza ujuzi wao, kufanya kazi kwa pamoja na kubuni suluhisho zinazotumia teknolojia na ambazo zinaweza kuwa na matokeo chanya katika jamii.

Hackathon ya mwaka huu itawakutanisha wanafunzi wa kike, wahitimu, wanaotarajia kuwa watengenezaji wa programu pamoja na wabunifu vijana, ambao watashirikiana katika timu, kupata ushauri kutoka kwa wataalamu na kuwasilisha suluhisho zao mbele ya jopo la majaji.

Washiriki watatakiwa kutumia fikra tunduizi, kutumia ujuzi wao wa kiteknolojia na kubuni mawazo mapya yanayoweza kuchangia katika mustakabali wa ajira, ujasiriamali na mageuzi ya kidijitali.

Mbali na mashindano, mpango huo utatoa jukwaa muhimu kwa wanawake vijana kupata uzoefu na uelewa zaidi kuhusu sekta ya teknolojia, kuunganishwa na wenzao pamoja na washauri, na kujenga kujiamini katika kutafuta ajira na fursa mbalimbali katika sekta hiyo.

Kwa washiriki wengi, uzoefu huo unaweza kuwa hatua ya kuingia katika programu za mafunzo kwa vitendo, ajira, ujasiriamali na kuendelea kujifunza katika teknolojia.
Oscar Mwamfwagasi

Akizungumzia umuhimu wa mpango huo, Ofisa Mkuu wa Uendeshaji wa Benki ya Absa Tanzania, Oscar Mwamfwagasi, alisema ushiriki wa waanzilishi wa biashara ndogo na za kati (SMEs) ni moja ya mambo yanayoongeza thamani katika Hackathon ya mwaka huu.

Kinachofanya Hackathon ya mwaka huu kuwa na thamani zaidi ni ushiriki wa moja kwa moja wa waanzilishi wa biashara ndogo na za kati, ambao wanaleta uzoefu wa vitendo katika biashara pamoja na changamoto halisi zinazokabili biashara kwenye programu hii.”

Alisema ushiriki wao unasaidia kuboresha safari ya kujifunza kwa washiriki, huku ukifungua fursa kwa kampuni changa kuonyesha mawazo yao, kupata mwongozo kutoka kwa wataalamu wa sekta mbalimbali na kujenga mahusiano yanayoweza kusaidia kuharakisha ukuaji wa biashara zao.

Programu kama hii ni muhimu katika kukuza ubunifu, kuwawezesha wajasiriamali na kujenga mfumo jumuishi zaidi wa kidijitali unaosaidia maendeleo endelevu ya Afrika,” alisema Mwamfwagasi.

Kadiri GirlCode Hackathon inavyoendelea kukua katika mataifa mbalimbali ya Afrika, Tanzania imeendelea kuwa mfano wa kile kinachoweza kufikiwa pale wanawake vijana wanapopewa majukwaa, rasilimali na mitandao sahihi ya kuwawezesha.

Ushindi wa Tanzania katika mashindano ya Pan-African mwaka 2025 umeweka msingi imara, huku toleo la mwaka huu likilenga kutoa hamasa kwa kizazi kijacho cha wanawake wa Tanzania wanaotaka kujikita katika teknolojia kufikia mafanikio makubwa zaidi.

GirlCode imewahimiza wanawake vijana nchini Tanzania, wadau, walezi na washiriki wa mfumo wa teknolojia kuunga mkono Hackathon ya mwaka huu na kushirikiana katika kujenga mustakabali wa kidijitali unaojumuisha watu wengi zaidi barani Afrika.

GirlCode Tanzania Hackathon 2026 itafanyika tarehe 26–27 Septemba 2026.

Share:

PROF. KABUDI AWATAKA WANANCHI KUZINGATIA TAHADHARI ZA MAAFA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amewataka wananchi kuzingatia tahadhari na maelekezo yanayotolewa na wataalamu na mamlaka husika ili kupunguza madhara yanayotokana na majanga na maafa.

Prof. Kabudi ametoa wito huo tarehe 19 Agosti, 2026 wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Watoa Huduma za Misaada ya Kibinadamu Duniani yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Ushiriki wa wananchi ni muhimu katika kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya majanga, huku akiwataka kuendelea kufuata taarifa na maelekezo rasmi kutoka kwa wataalamu na mamlaka zinazohusika na masuala ya maafa.

Katika hatua nyingine, alisema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema na kujenga ustahimilivu wa jamii ili kuongeza uwezo wa wananchi kukabiliana na majanga na kupunguza madhara yanayotokana na matukio hayo.

Alisema uwezo wa nchi katika kukabiliana na majanga kwa ufanisi unategemea uwepo wa mifumo madhubuti, uratibu na ushirikiano wa karibu na wenye tija kati ya Serikali na wadau wa huduma za kibinadamu.

Prof. Kabudi pia alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake katika kusimamia masuala ya kibinadamu na ustawi wa wananchi.

Kupitia uongozi wa Rais Dkt. Samia, Serikali imeendelea kuhakikisha wananchi wanaokumbwa na changamoto za majanga wanapata msaada na faraja wakati wa dharura.

Prof. Kabudi aliwataka watoa huduma za kibinadamu kuwekeza zaidi katika kuwawezesha wananchi kwa elimu na taarifa sahihi kuhusu vihatarishi vinavyowazunguka, pamoja na hatua za kuchukua kabla, wakati na baada ya janga.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. James Kilabuko, amesema maadhimisho ya siku hiyo yanatoa fursa ya kutambua na kuthamini mchango wa watoa huduma za kibinadamu ambao hujitolea kwa moyo wa huruma, ujasiri na mshikamano katika kuokoa maisha na kupunguza madhara.

Alisema ni muhimu kuendelea kuimarisha ushirikiano na mshikamano miongoni mwa Serikali, wadau wa huduma za kibinadamu na jamii katika kuhakikisha kuwa msaada unapatikana kwa wakati na unawafikia wale wanaouhitaji.

Ni muhimu kuhakikisha kuwa katika kila hatua ya utoaji wa huduma za kibinadamu, maisha, usalama na utu wa mwanadamu vinaendelea kuwa kiini cha hatua tunazochukua.
Share:

BENKI YA ABSA YAZINDUA “ABSA LIPA SASA” KUKUZA MALIPO YA KIDIJITALI NA UJUMUISHAJI WA HUDUMA ZA KIFEDHA

Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa, Bw. Victor Nchimbi (wa tano kushoto), Meneja Masoko, Mawasiliano na Chapa, Bw. Beda Biswalo (wa nne kushoto) na Meneja Bidhaa Kitengo cha Biashara, Bi. Devroda Kagusa (wa tatu kulia), pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa benki hiyo, wakizindua mfumo wa malipo wa Absa Lipa Sasa, wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo. Kupitia Absa Lipa Sasa, wateja wanaweza kulipa kutoka benki au mtandao wowote kwa kutumia QR code au lipa namba hivyo kurahisisha malipo kwa kutumia njia za kidigitali.

Benki ya Absa Tanzania imezindua rasmi Absa Lipa Sasa, huduma mpya ya malipo ya kidijitali inayotumia mfumo wa TanQR, ikiwa na lengo la kuwawezesha wafanyabiashara na watumiaji kufanya malipo kwa haraka, usalama na urahisi kupitia mfumo mmoja unaokubalika na benki mbalimbali pamoja na mitandao ya simu nchini.

Huduma hiyo imejengwa kwa kuzingatia kiwango cha kitaifa cha TanQR chini ya usimamizi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), na inawawezesha wafanyabiashara kupokea malipo kutoka benki mbalimbali na mitandao ya simu kwa kutumia QR Code moja, hivyo kurahisisha miamala na kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Victor Nchimbi, alisema huduma hiyo imeundwa kurahisisha malipo kwa wafanyabiashara na wateja wao.

Kupitia Absa Lipa Sasa, mfanyabiashara anahitaji QR Code moja tu kupokea malipo kutoka kwa wateja wanaotumia benki tofauti au mitandao mbalimbali ya simu. Hii inaondoa ulazima wa kutumia vifaa au mifumo mingi ya malipo, hivyo kupunguza gharama za biashara, kuongeza kasi ya miamala, kuboresha utunzaji wa kumbukumbu na kuimarisha usalama wa malipo. Kwa wateja, huduma hii inaleta uzoefu rahisi, salama na unaotegemewa wa kufanya malipo ya kidijitali,” alisema Nchimbi.

Alieleza kuwa uzinduzi wa huduma hiyo unaunga mkono juhudi za Serikali ya Tanzania za kuongeza ujumuishaji wa huduma za kifedha na kuharakisha matumizi ya teknolojia katika shughuli za kiuchumi kupitia mifumo ya malipo ya kidijitali.

Kwa kutumia uwezo wa mfumo wa TanQR, Absa Lipa Sasa inawawezesha wafanyabiashara kupokea malipo yote kupitia mfumo mmoja bila kuwa na ulazima wa kutumia mifumo au vifaa tofauti vya malipo.

Akizungumza zaidi kuhusu faida za huduma hiyo Nchimbi alisema QR Code hiyo moja inakubali malipo kutoka benki mbalimbali na mitandao ya simu huku uthibitisho wa miamala ukipatikana papo hapo.

Aliongeza kuwa mfumo huo unapunguza utegemezi wa fedha taslimu, kuongeza uwazi katika miamala ya malipo na kupunguza gharama za kupokea malipo, hususan kwa biashara ndogo, za kati na za kati zinazokua (MSMEs).

"Huduma hiyo inalenga kuwahudumia wafanyabiashara wadogo, wa kati na wakubwa, pamoja na wafanyabiashara wa sekta isiyo rasmi wanaohitaji njia salama, rahisi na yenye ufanisi ya kupokea malipo", aliongeza.

Kwa upande wake, Meneja Masoko, Mawasiliano na Chapa wa Benki ya Absa Tanzania, Beda Biswalo, alisema uzinduzi wa Absa Lipa Sasa unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuwasaidia wateja kufikia malengo yao kupitia suluhisho bunifu za malipo.

Katika Absa tunaamini kuwa ‘Stori Yako Ina Thamani’ kwa sababu kila mteja, mjasiriamali na biashara ina ndoto zinazostahili kuungwa mkono. Absa Lipa Sasa inaonesha dhamira yetu ya kuwasaidia wateja wetu kukua kupitia huduma rahisi, salama na zinazopatikana kirahisi ambazo zinakidhi mahitaji yao ya kila siku. Hivi ndivyo tunavyotekeleza lengo letu la ‘Kuiwezesha Afrika ya Kesho, Pamoja… Hatua Moja Baada ya Nyingine,’ huku tukichochea ujumuishaji wa huduma za kifedha na mageuzi ya kidijitali nchini Tanzania,” alisema Biswalo.

Kupitia Absa Lipa Sasa, wafanyabiashara watapanua wigo wa wateja wao, kupunguza hatari zinazotokana na matumizi ya fedha taslimu, pamoja na kujenga historia ya miamala ya kidijitali ambayo inaweza kusaidia kupata huduma nyingine za kifedha siku zijazo.

Huduma hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa Benki ya Absa Tanzania wa kuendeleza mageuzi ya kidijitali na kuimarisha nafasi yake kama mshirika wa kuaminika wa kifedha na taasisi inayochangia maendeleo chanya ya jamii.

Absa Lipa Sasa imeanza kupatikana kwa wafanyabiashara kote nchini, ambapo usajili unaweza kufanyika katika matawi yote ya Benki ya Absa Tanzania au kupitia wasimamizi wa mahusiano ya wateja wa benki hiyo.
Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa, Bw. Victor Nchimbi (katikati), Meneja Masoko, Mawasiliano na Chapa, Bw. Beda Biswalo (kushoto) na Meneja Bidhaa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa wakifanya malipo kwa simu kwa kutumia mfumo wa malipo wa Absa Lipa Sasa, wakati wa uzinduzi wa mfumo huo jijini Dar es Salaam leo. Kupitia Absa Lipa Sasa, wateja wanaweza kulipa kutoka benki au mtandao wowote kwa kutumia QR code au lipa namba hivyo kurahisisha malipo kwa kutumia njia za kidigitali.
Share:

TANZANIA YAZINDUA UWANJA WA KISASA WA KRIKETI, ICC YAIONA TAYARI KWA MASHINDANO YA KIMATAIFA


Mwenyekiti wa Shirikisho la Kimataifa la Kriketi (ICC), Jay Shah (katikati), akiongoza uzinduzi wa Uwanja wa Kisasa wa Chama cha Kriketi Tanzania (TCA Cricket Arena) uliojengwa katika Viwanja vya Michezo vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Uwanja huo utatumika kama kituo cha taifa cha kukuza vipaji na kuandaa timu za taifa za wanaume, wanawake na vijana wenye umri wa chini ya miaka 19. Wengine pichani ni wadau wa mchezo wa kriketi.

DAR ES SALAAM – Shirikisho la Kimataifa la Kriketi (International Cricket Council - ICC) limesema Tanzania ina nafasi ya kuwa miongoni mwa mataifa yatakayoweza kuandaa mashindano makubwa ya kriketi duniani siku zijazo, kufuatia uwekezaji unaoendelea katika miundombinu ya kisasa ya mchezo huo na maendeleo ya vijana.

Kauli hiyo imetolewa wakati wa uzinduzi wa Uwanja wa Kisasa wa Chama cha Kriketi Tanzania (TCA Cricket Arena), uliojengwa katika viwanja vya michezo vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Uwanja huo utatumika kama kituo cha taifa cha kukuza vipaji na kuandaa timu za taifa za wanaume, wanawake na vijana wenye umri wa chini ya miaka 19.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi, Mwenyekiti wa ICC, Jay Shah, alisema Tanzania imeonyesha dhamira kubwa ya kuendeleza mchezo wa kriketi kupitia uwekezaji katika miundombinu na programu za maendeleo ya vijana, hatua ambayo imeifanya kuwa miongoni mwa mataifa yanayokua kwa kasi katika mchezo huo barani Afrika.

Alisema iwapo kasi hiyo ya maendeleo itaendelea, Tanzania inaweza kuwa miongoni mwa nchi zitakazopewa fursa ya kuandaa mashindano makubwa ya kimataifa, ikiwemo Kombe la Dunia la Kriketi, katika miaka ijayo.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Chama cha Kriketi Tanzania (Tanzania Cricket Association - TCA), Hamisi Hassan Abdallah, alisema uwanja huo mpya utaongeza uwezo wa Tanzania kuandaa mashindano ya kimataifa huku ukiwapatia wachezaji mazingira bora ya mazoezi yanayokidhi viwango vya kimataifa.

Alibainisha kuwa kwa muda mrefu TCA ilikuwa na uwanja mmoja pekee, hali iliyokuwa ikizuia juhudi za kuandaa mashindano makubwa kutokana na uhaba wa miundombinu inayokidhi matakwa ya mashirikisho ya kimataifa.

Naye Afisa Mwandamizi wa Michezo kutoka Baraza la Michezo la Taifa (NSC), Apansia Lema, alisema Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya michezo ili kuibua na kukuza vipaji vya vijana nchini.

Alisema maendeleo ya mchezo wa kriketi yanaendelea kuimarika, huku zaidi ya shule 400 nchini zikishiriki mchezo huo. Aidha, alitaja kufuzu kwa timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 19 kushiriki Kombe la Dunia la Kriketi 2026 kuwa mafanikio makubwa yanayoonyesha mwelekeo mzuri wa maendeleo ya mchezo huo nchini.

Uzinduzi wa TCA Cricket Arena unatarajiwa kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha kriketi katika ukanda wa Afrika Mashariki na kuongeza uwezo wa nchi kuvutia mashindano ya kimataifa, kuendeleza vipaji vya vijana na kukuza utalii wa michezo.


Share:

BENKI YA ABSA NA KNAUF GYPSUM TANZANIA WAUNGANISHA NGUVU KUWEZESHA WASAMBAZAJI KUPATA MITAJI

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw Obedi Laiser (kulia), na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania, Bw. Christoforos Stamoulakatos, wakisaini Hati za Makubaliano (MoU) yenye lengo la kuanzisha Mpango wa Ufadhili kwa Wasambazaj, hatua inayolenga kuwawezesha wasambazaji wa Knauf kupata mitaji ya biashara kwa urahisi zaidi, kuimarisha mnyororo wa ugavi na kuchochea ukuaji wa sekta ya ujenzi nchini. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Meneja wa Sheria na Mahusiano ya Nje na Serikali wa Knauf, Bi. Flora Erasto na kulia ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi.

BENKI ya AbsaTanzania na Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania zimesaini Hati ya Makubaliano (MoU) ya kuanzisha Mpango wa Ufadhili kwa Wasambazaji (Distributor Financing Programme), hatua inayolenga kuwawezesha wasambazaji wa Knauf kupata mitaji ya biashara kwa urahisi zaidi, kuimarisha mnyororo wa ugavi na kuchochea ukuaji wa sekta ya ujenzi nchini.

Kupitia makubaliano hayo, Benki ya AbsaTanzania itatoa huduma maalum za kifedha kwa wasambazaji watakaokidhi vigezo vya benki, ikiwa ni pamoja na mikopo ya mtaji wa biashara na ufadhili wa ununuzi wa bidhaa. Awamu ya kwanza ya mpango huo inatarajiwa kuwahusisha wasambazaji kati ya 30 na 40 kutoka mtandao wa Knauf nchini Tanzania.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini iliyofanyika katika makao makuu ya Knauf Gypsum Tanzania jijini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki AbsaTanzania, Bw. Obedi Laiser alisema, ushirikiano huo unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kutumia huduma za kifedha kuimarisha biashara na kuongeza thamani katika mnyororo mzima wa biashara.

"Ushirikiano huu unaonesha nguvu ya mfumo shirikishi wa huduma za kibenki katika kusaidia ukuaji wa biashara na kuleta manufaa kwa wadau wote. Kwa kuwapatia wasambazaji wa Knauf suluhisho za kifedha, tunawawezesha kuongeza uwezo wao wa biashara, kuboresha ufanisi na kutumia kikamilifu fursa za ukuaji. Absa tunaendelea kutekeleza dhamira yetu ya kuiwezesha Afrika ya kesho, pamoja, hatua moja baada ya nyingine," alisema Bw. Laiser.

Alisema mpango huo utawapa wasambazaji uwezo wa kupata mitaji ya kuendesha biashara, kuongeza akiba ya bidhaa na kupanua shughuli zao, jambo litakaloimarisha upatikanaji wa bidhaa za Knauf katika soko la Tanzania.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Knauf Gypsum Tanzania, Bw. Christoforos Stamoulakatos, alisema ushirikiano huo utawajengea uwezo wasambazaji wa kampuni hiyo na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wateja.

"Wasambazaji wetu ni sehemu muhimu ya mafanikio ya kampuni yetu na uwezo wetu wa kuwahudumia wateja kote nchini. Kupitia ushirikiano huu na Absa Bank Tanzania, tunawapa fursa ya kupata huduma za kifedha zitakazowasaidia kukuza biashara zao na kukidhi mahitaji yanayoendelea kuongezeka sokoni," alisema.

Mpango huo unaendana na mkakati wa Benki ya Absa Tanzania wa mfumo shirikishi wa huduma za kibenki unaolenga kutoa huduma jumuishi za kifedha zinazosaidia mnyororo mzima wa thamani kwa kuwaunganisha wazalishaji, wasambazaji na wadau wengine wa biashara kupitia suluhisho bunifu za kifedha.

Knauf Gypsum Tanzania ni mmoja wa wateja wakubwa wa Benki ya Absa Tanzania katika kitengo cha Wateja wa Makampuni (CIB), na kampuni hiyo imeendelea kuwa mdau muhimu katika sekta ya ujenzi nchini. Kupitia mpango huo mpya, taasisi hizo zinatarajia kuimarisha zaidi ushirikiano wao na kufungua fursa mpya za ukuaji wa biashara kwa wadau wote.

Hafla ya utiaji saini ilihudhuriwa na viongozi wakuu wa Benki ya Absa Tanzania na Knauf Gypsum Tanzania, wasambazaji, washirika wa biashara pamoja na wawakilishi wa vyombo mbalimbali vya habari.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw Obedi Laiser (kulia), na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania, Bw. Christoforos Stamoulakatos, wakibadilishana Hati za Makubaliano (MoU), katika hafla ya utiaji saini makubaliano hayo, yenye lengo la kuanzisha Mpango wa Ufadhili kwa Wasambazaji, hatua inayolenga kuwawezesha wasambazaji wa Knauf kupata mitaji ya biashara kwa urahisi zaidi, kuimarisha mnyororo wa ugavi na kuchochea ukuaji wa sekta ya ujenzi nchini. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Meneja wa Sheria na Mahusiano ya Nje na Serikali wa Knauf, Bi. Flora Erasto na kulia ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw Obedi Laiser, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania, Bw. Christoforos Stamoulakatos, wakipiga picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi kutoka pande zote mbili katika hafla ya utiaji saini hati za makubaliano (MoU), yenye lengo la kuanzisha Mpango wa Ufadhili kwa Wasambazaji, hatua inayolenga kuwawezesha wasambazaji wa Knauf kupata mitaji ya biashara kwa urahisi zaidi, kuimarisha mnyororo wa ugavi na kuchochea ukuaji wa sekta ya ujenzi nchini. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw Obedi Laiser (kulia), akimsikiliza moja wa wateja wa Kampuni ya Knauf ambaye ni Mkurugenzi wa Kichomo General Traders, Bw. Hamad Msellem Hassan (wa pili kushoto), mara baada ya utiaji saini hati za makubaliano (MoU), na Knauf yenye lengo la kuanzisha Mpango wa Ufadhili kwa Wasambazaji, hatua inayolenga kuwawezesha wasambazaji wa Knauf kupata mitaji ya biashara kwa urahisi zaidi, kuimarisha mnyororo wa ugavi na kuchochea ukuaji wa sekta ya ujenzi nchini. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo.
Share:

BENKI ZA ABSA NA TCB KUIMARISHA MAHUSIANO YA USHIRIKIANO WA KIMKAKATI

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akisalimiana na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake, jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto), akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo (kushoto), pamoja na baadhi ya maofisa wa benki hiyo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa nne kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo (wa tano kushoto), pamoja na baadhi ya maofisa kutoka benki zote mbili, wakipiga picha ya kumbukumbu mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kutembelea ofisini za TCB, jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.
Share:

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

LILIAN-FAVOUR MAKAWA

Popular Posts

Blog Archive

Labels

Blog Archive

Recent Posts

Label Cloud

BIASHARA (334) BURUDANI (4) KIMATAIFA (10) KITAIFA (131) MICHEZO (41) SIASA (3)

Pages